Wednesday, May 08, 2013

DIWANI NA MTENDAJI WASHIKILIWA KWA TUHUMA YA MAUAJI

JESHI la polisi mkoani Kagera linamshikilia diwani wa kata ya Rutoro Abubakar Saidi na watu wengine  sita akiwemo afisa mtendaji wa kata ya Rutoro Japhet Kuyeyumba kwa  kuhusika na tuhuma ya kuwaua watu  wanne kwa nyakati tofauti ambao ni walinzi wa wawekezaji waliorasimishwa eneo la ardhi  ya ranchi ya Kagoma ya kwa ajili ya ufugaji wa kisasa na wa kibiashara.
 
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake kaimu kamanda wa jeshi la polisi mkoani Kagera, kamishina msaidizi wa jeshi  hilo Henry Mwaibambe alisema wanaoshikiliwa wanatuhumiwa kufanya mauaji ya watu hao kati ya mei 17 na mei 18, mwaka huu.
 
Alisema tukio la kwanza la mauaji  lilitokea mei 17 katika kitongoji cha Rwamisha, kijiji na kata ya Rutoro wilayani Muleba ambapo kundi la watu wanaokadiriwa kuwa kati ya 50 wakiwa na silaha za jadi na mapanga wakiongozwa na diwani anayeshikiliwa na jeshi la polisi walimuua kwa kumkata koromeo mchunga Ng’ombe James Venus (20) mlinzi wa kitalu namba 9 kinachomilikiwa na Faustin Rutaoile.
 
Mwaibambe alisema diwani huyo anatuhumiwa kuwahamasisha wananchi  wamuue mchungaji huyo kwa madai kuwa ameachia ng’ombe wa mwekezaji huyo  aliokuwa anawachunga wakaingia  kwenye shamba la mtu mmoja aliyetajwa kwa jina moja la James kuharibu mazao yake.
 
Aliendelea kusema kuwa tukio la pili lilitokea mei 18, mwaka huu majira ya mchana ambapo wananchi wale wale wakiongozwa na diwani huyo waliwaua walinzi watatu baada ya kuwazingira ambao aliwataja kuwa ni pamoja Mhidin Yassin, Amos Richard na mwingine aliyemtaja kwa jina moja la Mugisha.
 
Kaimu kamanda huyo alisema kuwa katika tukio hilo la pili mmoja wa walinzi aliyekuwa na bunduki aina ya shortgun  alimuua  mwananchi mmoja aliyemtaja kwa jina la Said Ndyanabo (35) katika harakati za kujiokoa na hivyo kufanikiwa kutoroka toka mikononi mwa wauaji.
 
Alisema mauaji yote yalitekelezwa kwa staili ya pekee ambapo wauaji walikuwa wakiwaua walinzi kwa kuwakata  makoromeo na kuwakata sehemu mbalimbali za miili yao.
 
Alimaliza kwa kuwaambia waandishi wa habari kuwa uchunguzi wa awali  unaonyesha kuwa mauaji yote yaliyotekelezwa yalikuwa yamepangwa chini uongozi wa mheshimkiwa diwani ambaye jeshi la polisi linamshikilia kwa kushirikiana na baadhi ya viongozi wa ngazi ya kijiji cha Rutoro.
 
Watuhumiwa wengine wanaoshikiliwa na jeshi la polisi kwa tuhuma ya kuhusika na mauaji ni pamoja na James Kabeba (51), Andrew Lucas (45), Dawson Sylivester (26), Ernest Reuben na Ancheleus Kahatano (65) wote wakazi wa kijiji na kata ya Rutoro.

No comments:

Post a Comment