Tuesday, July 19, 2016

MAJALIWA: MALIASILI NA UTALII JIPANGENI VIZURI



WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ameiagiza Wizara ya Maliasili na Utalii
kujipanga vizuri na kufanya mapitio ya idara zake hususan ya misitu baada ya kubainika kuwepo kwa matatizo makubwa.
“Eneo la misitu limekuwa na matatizo makubwa, watendaji wengi si waaminifu na sura ya wizara si nzuri miti mingi inakatwa na fedha haiingii Serikalini. Huu ni mgogoro mpya,” alisema.
Waziri Mkuu ametoa agizo hilo jana alipokutana na watumishi wa wizara hiyo jana (Jumatatu, Julai 18, 2018) jijini Dar es Salaam, na kusisitiza kwamba hakuna sababu ya Serikali kuendelea kuwa na watumishi wasiokuwa na uaminifu, uadilifu na uwajibikaji.
Alisema lengo la mkutano huo ni kukutana na watumishi
kusikiliza changamoto zao, kukumbushana wajibu, pamoja na kutoa maagizo ili
yatekelezwe kwa utaratibu unaokubalika kisheria.

Alisema mtumishi ambaye atabainika kuwa haitendei haki nafasi yake kwa
kutokutimiza majukumu ipasavyo hana sababu ya kuwepo kwa sababu serikali
inapoteza fedha nyingi kuwalipa watu wasio na tija.

Waziri Mkuu alisema sababu inayoikosesha Serikali mapato ni
uwepo wa watumishi wasio waadilifu kwenye ofisi za Serikali ikiwemo Wizara
ya Maliasili na Utalii hivyo kuna umuhimu wa kuzisafisha.

Alisema kuna uvunaji mkubwa wa misitu kuliko upandaji huku asilimia 50 ya mapato yatokanayo na uvunaji huo yanapotea na kuisababishia Serikali hasara ambapo alihoji sababu ya wizara kushindwa kusimamia jambo hilo.

Katika hatua nyingine; Waziri Mkuu aliitaka wizara hiyo kupunguza idadi ya vizuizi vya ukaguzi wa mazao ya
misitu kwenye barababara mbalimbali baada ya kukosa tija kutokana na upotevu wa misitu unaotokea kila siku.

Alitoa mfano wa barabara ya kwenda mikoa ya kusini  kuanzia Dar es Salaam
ambapo alisema ina vizuizi visivyopungua sita na kila kizuizi kinatumika kwa ajili ya kukagua mazao ya misitu na maliasili inayotoka kuvunwa.

“Vizuizi vya katikati ya safari havina umuhimu na badala yake kuwe
na vizuizi mwanzo na mwisho ili rasilimali zingine zitumike kuongeza nguvu
na umakini wa ukaguzi kwenye vituo vichache vitakavyosalia,”.

“Kwa mfano ukitokea Ikwiriri kuja Dar, kuna vituo vya ukaguzi wa maliasili
visivyopungua sita, kuna Ikwiriri, Kibiti,  Jaribu Mpakani,Mkuranga, Vikindu  kote huku
wanakagua lakini linapofika kituo cha mwisho cha Mbagala linakutwa na makosa kwenye mzigo kwanini’’?

“Yule mkaguzi wa kwanza alifanya kazi gani? Kuna tatizo la uadilifu na
ninyi ni mashahidi, sasa naagiza ongezeni nguvu kwenye vituo vikuu vya
ukaguzi yaani mwanzo na mwisho,” alisema.

Aidha alisema ni muhimu kukawa na mabadiliko kwenye mfumo wa mauzo ya
misitu kutoka wa sasa (kuuza kwa eneo) na kuhamia kwenye mfumo wa mnada
ambao utaongeza mapato ya Taifa na utaweka uwazi.

Pia aliwataka watumie mashine za malipo za kielektroniki (EFD),wanapofanya mauzo ya mazao ya misitu ili
kuepusha matumizi ya daftari na risiti bandia ambazo hazitambuliwi na
wizara.

MAJALIWA: BARA LA AFRIKA BADO LINAKABILIWA NA CHANGAMOTO YA UPATIKANAJI WA MAJI


WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Bara la Afrika bado linakabiliwa na changamoto ya upatikanaji wa maji safi na salama hasa vijijini kwa sababu nchi zake bado hazijamudu kuunganisha huduma hiyo katika maeneo hayo.
Kufuatia hali hiyo, Waziri Mkuu amewataka wataalamu wa masuala ya maji watafute njia sahihi itakayowezesha kutatua tatizo hilo kwa kutumia vyanzo mbalimbali vya maji vilivyoko.
Waziri Mkuu alitoa kauli hiyo jana (Jumatatu, Julai 18, 2016) katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere  jijini Dar es salaam wakati akifungua mkutano wa 10 wa Baraza la Mawaziri wa Maji wa Afrika (AMCOW) ambao unaokwenda sambamba na maadhimisho ya Wiki ya Maji Afrika.
“Tunategemea baada ya kumazika kwa mkutano huu wataalamu wetu wataondoka na maazimio mazuri ya kumaliza tatizo la maji katika Bara letu kwa kutumia mito na maziwa ili kufikisha maji kwa wananchi,” alisema.
Akizungumzia kwa upande wa Tanzania alisema,  suala la maji limepewa kipaumbele hata katika bajeti ya mwaka huu na kwamba Serikali itahakikisha maji yanapatikana katika maeneo yote ili kutimiza sera yake ya kila mwananchi kupata maji umbali usiozidi mita 400.
Kwa upande wake Rais Mstaafu wa Kenya Mwai Kibaki ambaye ni Mjumbe Maalumu wa UNESCO kwa ajili ya masuala ya maji Barani Afrika alisema maji ni muhimu kwa maendeleo ya uchumi, hivyo wataalamu wanatakiwa kuhakikisha huduma hiyo inapatika katika maeneo yote.
Mkutano huo  wa siku tano unahudhuriwa Mawaziri wa Maji kutoka nchi 45 za Afrika na unaongozwa na Waziri wa Maji na Mazingira wa Senegal Amadou Mansour Faye ambaye ni Rais wa AMCOW.
(mwisho)
 

NSSF YACHANGIA MILIONI 50 HARAMBEE YA UJENZI MPYA WA LINDI SEKONDARI


Shirika la Hifadhi ya Taifa ya Jamii NSSF Makao Makuu ikishirikiana na Ofisi ya Mkoa wa Lindi Imechanga Jumla ya Shilingi Milioni 50 Kwa Ajili ya Kuchangia Harambee ya Kusaidia Ujenzi wa Shule ya Sekondari ya Lindi Iliyoungua Moto Wiki Iliyopita
Kwa Kutambua Umuhimu wa Elimu kwa  Watoto Shirika Hilo Kupitia Mkurugenzi Mkuu Wake ,Aliewakilishwa na Meneja wa Mkoa Bi Nour Aziz Limetoa ahadi hiyo kwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Majaliwa Kasim Majaliwa Alieongoza Harambee Hiyo Ambayo Ilihudhuriwa na Wadau Mbali mbali Akiwemo Mke wa Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne,Mama Salma Kikwete
Katika Harambee Hiyo Jumla ya Shilingi Milioni 80 Taslimu zilichangwa Huku Ahadi na Vifaa vya Ujenzi zikifikia Shilingi Milioni 640 Ambapo Katika Ujenzi Mpya Waziri Mkuu Ameagiza Kujengwa Jengo la Ghorofa litakalokuwa na Ofisi na  Madarasa
Katika Tukio Hilo la Moto,Jumla Ya Madarasa 9 na viti na Meza zaidi ya 300,Ofisi 4 na Vyoo Matundu 24  Viliteketea na Moto Uliotokana na hitilafu ya Umeme

MAJALIWA: MARUFUKU WANAFUNZI KUTUMIA VIBERITI, MISHUMAA MABWENINI


WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amepiga marufuku matumizi ya viberiti, mishumaa na hita za kuchemshia maji kwa wanafunzi wa bweni ili kuepusha majanga ya moto na atakayekutwa atachukuliwa hatua kali.
“Kuna tabia ya baadhi ya wanafunzi hasa wa masomo ya fizikia kutengeneza vifaa vya kienyeji vya kuchemsha maji mabwenini jambo hili ni la hatari kwani linaweza kusababisha ajali ya moto, hivyo ni marukufu kwa mwanafunzi kutumia vifaa hivyo,” alisema.
Waziri Mkuu ametoa agizo hilo leo (Jumapili, Julai 17, 2016) katika harambee ya kuchangisha fedha za ujenzi wa majengo ya shule ya sekondari Lindi yaliyoungua moto usiku wa kuamkia Julai 10 mwaka huu.
Katika ajali hiyo shule imeathirika kwa asilimia 34 ambapo vyumba tisa vya madarasa, jengo lenye matundu 26 ya vyoo na jengo la maabara ya kemia na fizikia yameungua na kusababishia hasara ya sh. milioni 682.78.
Waziri Mkuu amesema kwa namna ambavyo majengo hayo yameungua ni vema yakavunjwa na kujengwa upya ambapo aliwataka kutumia nafasi hiyo kwa kujenga jengo la ghorofa ili kutumia eneo dogo kwa kujenga madarasa mengi.
Pia alimuagiza Mkuu wa mkoa wa Lindi, Godfrey Zambi kuhakikisha fedha zitakazopatikana katika harambee hiyo zinatumika kama ilivyokusudiwa.
Harambee ilihudhuriwa na mke wa Waziri Mkuu, Mary Majaliwa, mke wa Rais mstaafu wa awamu ya nne, mama Salma Kikwete, mkuu wa mkoa wa Mtwara, Halima Dendego pamoja na wadau wa maendeleo na wanafunzi waliosoma shule hiyo akiwemo Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhandisi Ramo Makani.
Katika hatua nyingine Waziri Mkuu amezitaka taasisi mbalimbali nchini kufunga vifaa vya kuzimia moto katika majengo yao kwa ajili ya kuvitumia pindi ajali za moto zinapotokea.
(mwisho)
 IMETOLEWA NA:

Tuesday, March 08, 2016

WAZIRI MKUU: RUSHWA YAPOTEZA DOLA BILIONI 150 AFRIKA



WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema tatizo la rushwa barani Afrika limesababisha bara hilo lipoteze dola za Marekani bilioni 150 kila mwaka.

Ametoa kauli hiyo leo mchana (Jumanne, Machi 8, 2016) wakati akihutubia wajumbe wa mkutano wa tano wa Bunge la Afrika Mashariki (EALA) linaloendesha vikao vyake jijini Dar es Salaam. Mkutano huo ulioanza Machi 6, utamalizika Machi 18, mwaka huu.

Akizungumza kwa niaba ya Rais Dk. John Pombe Magufuli, Waziri Mkuu alisema rushwa imechangia kwa kiasi kikubwa kurudisha nyuma maendeleo ya Jumuiya hiyo. "Rushwa yaweza kuwa kwa njia kuhonga fedha, kupata fedha kwa kula njama, kujipatia fedha kwa njia za udanganyifu, ama kwa njia za vitisho," alisema.

"Kwa mujibu wa taarifa ya Umoja wa Afrika (AU), rushwa na urasimu vimeainishwa kuwa ni vikwazo vikubwa vinavyochangia kuchelewesha ufanyaji wa biashara kwenye mipaka ya nchi za Jumuiya yetu," alisema.

Amesema sekta binafsi inachukuliwa kama injini ya maendeleo na ukuaji wa uchumi na akatumia fursa hiyo kuipongeza jumuiya ya wafanyabiashara wa Afrika Mashariki kwa kuandaa kanuni za kiutendaji  ambazo zimelenga kuhamasisha uadilifu kwenye ufanyaji biashara unaozingatia haki za binadamu, sheria za kazi, utunzaji mazingira na vita dhidi ya rushwa.

Akizungumzia kuhusu uondoaji wa vikwazo visivyohusisha kodi (non-tariff barriers) kama njia mojawapo ya kuimarisha biashara kwenye jumuiya hiyo, Waziri Mkuu alisema kwa upande wa Tanzania, vizuizi vya barabarani kwenye barabara kuu ya Kaskazini vimepunguzwa kutoka 50 hadi vitano.

Alivitaja vizuizi vitano vilivyobakia kuwa ni vile vilivyopo kwenye mizni ya Mikese (Morogoro), Nala (Dodoma), Njuki (Singida), Mwendakulima (Shinyanga) na Nyakahura (Kagera).

"Sheria ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya uondoaji wa vikwazo visivyohusisha kodi ilipitishwa Machi 2015 na sasa hivi inaendelea kusainiwa na Wakuu wa Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki. Pamoja na mambo mengie, nia ya sheria hii ni kuondoa vikwazo vinavyosababisha uagizaji wa bidhaa kutoka nje ya nchi na uuzaji wa bidhaa nje ya nchi, kurahisisha sheria za biashara ndani ya Jumuiya yetu," alisema.

Akizungumzia kuhusu miradi ya uwekezaji ya Jumuiya hiyo, Waziri Mkuu alisema miradi ya ujenzi wa barabara inahitaji kiasi cha dola za marekani bilioni 20; ukarabati na upanuzi wa njia za reli unahitaji dola za marekani bilioni 30; uendeshaji wa mashirika ya ndege na viwanja vya ndege unahitaji dola za marekani bilioni 15; uendelezaji bandari na usafiri wa majini unahitaji dola za marekani bilioni 10; utekelezaji wa miundombinu ya nishati inahitaji dola bilioni 5 ambavyo kwa pamoja vinahitaji dola marekani bilioni 80.

Alisema kuwepo kwa shughuli mbalimbali za kiuchumi ndani ya jumuiya hiyo, kunaifanya Jumuiya ya Afrika Mashariki kuhesabika kuwa ni jumuiya yenye nguvu kubwa ya kiuchumi barani Afrika.


IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
2 MTAA WA MAGOGONI,
S.  L. P. 3021,
11410 DAR ES SALAAM.
JUMANNE, MACHI 8, 2016.

Saturday, February 13, 2016

SERIKALI YAWASIMAMISHA KAZI WATENDAJI WAKALA WA VIPIMO TANZANIA



SERIKALI imeamua kuwasimamisha kazi watendaji wawili kutoka Wakala wa Vipimo nchini (WMA) kuanzia leo ili kupisha uchunguzi wa upotevu wa mafuta bandarini kutokana na zuio la kufunga kwa mita kwa zaidi ya miaka mitano.

Waliosimamishwa kazi ni Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Vipimo nchini (WMA), Bi. Magdalena Chuwa na Meneja Vipimo Kitengo cha Bandari, Bi. Bernadina Mwijarubi. Bi. Mwijarubi ndiye anashughulikia kitengo cha mafuta bandarini.

Akitangaza uamuzi huo kwenye kikao cha Makatibu Wakuu kilichofanyika leo (Ijumaa, Februari 12, 2016) ofisini kwake Magogoni jijini Dar es Salaam, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amemwagiza Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara, Dk. Adelhelm Meru awaandikie barua za kuwasimamisha kazi ili kupisha uchunguzi huo.

“Katibu Mkuu Viwanda, waandikie barua za kuwasimamisha kazi ili kupisha uchunguzi. Katika kipindi hiki hawatatakiwa kusafiri kwenda popote hadi uchunguzi utakapokamilika. Pia utafute mtu wa kukaimu nafasi hiyo ili kazi ziendelee,” alisema.

Waziri Mkuu pia amesema ofisi yake itawaandikia barua ofisi ya TAKUKURU na polisi ili wafuatilie suala hilo mara moja na ikithibitika kuwa walihusika hatua rasmi zitachukuliwa na itathibitika hawakuhusika basi watarudishwa.

Waziri Mkuu pia aliagiza mfumo wa upimaji mafuta kwa kutumia flow meters uendelee kutumika na ule upimaji wa kukadiria uache kutumiwa mara moja.

Jana (Alhamisi, Februari 11, 2016) Waziri Mkuu alifanya ziara kukagua flow meters za zamani zilizopo Kurasini (Kurasini Oil Jetty) na kisha akatembelea na kukagua flow meters mpya ambazo zinajengwa Kigamboni. Mita hizo zimegharimu dola za marekani milioni 6 (sawa na sh. bilioni 12.96/- za sasa).

Pia Waziri Mkuu alitembelea sehemu ya kuchukulia mafuta yanayotoka bandarini (TPA Manfold) iliyoko Kigamboni na kukagua mitambo ya kusambazia mafuta kwenye matenki ya mafuta ya kampuni ya TIPER yaliyoko Kigamboni yanayomilikiwa kwa ubia baina ya Serikali na kampuni ya Oryx Energies.

Katika ziara hiyo ilibainika kuwa Kampuni ya TIPER imejiunganishia bomba la moja kwa moja kutoka kwenye bomba kubwa la mafuta linalotoka bandarini hali iliyomlazimu Waziri Mkuu kuagiza kwamba bomba hilo litolewe kwenye maungio hayo ndani ya mwezi mmoja.

“Jana niliagiza kuwa bomba hilo ling’olewe. Nimetoa mwezi mmoja ili kurekebisha mfumo huo. Simamieni vizuri na kuhakikisha kuwa na wao pia wanarudi kwenye manfold kama ilivyo kwa wengine,” alisema Waziri Mkuu.




IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
2 MTAA WA MAGOGONI,

WAZIRI MKUU AFANYA TENA ZIARA YA GHAFLA BANDARINI



*Aibukia kitengo cha mita za kupimia mafuta Kurasini
*Akuta mafundi wakizitengeneza, akuta zimejaa kutu
*Ataka barua ya maelezo ifikapo saa 11 leo jioni


WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amefanya ziara ya ghafla kwenye kitengo cha upimaji mafuta bandarini (Oil Flow Metres) na kukuta zimejaa kutu baada ya kutelekezwa kwa miaka zaidi ya mitano. Pia alitembelea mita za kupimia mafuta zinazoendelea kujengwa Kigamboni.

Aidha, Waziri Mkuu amempa saa nne tu Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Vipimo nchini (WMA), Bi. Magdalena Chuwa aandike barua ya kujieleza ni kwa nini aliamua kufunga mita hizo zisitumike kwa zaidi ya miaka mitano iliyopita na amletee barua hiyo ofisini kwake ifikapo saa 11 leo jioni.

“Nataka unieleze ni kwa nini ulitoa maelekezo ya kufunga mita hizo, na kwa nini jana uliamua kubadili uamuzi huo? Ni kwa nini umeamua kuchukua maamuzi haya baada ya kupokea ujumbe wa simu ya mkononi (sms) wakati mita zimekaa bila kufanya kazi kwa miaka mitano? Ni kwa nini umeamua kufanyia kazi ujumbe wa sms wakati unajua Serikali inafanya kazi kwa maandishi rasmi?” alisema Waziri Mkuu.

“Umesema mlikuwa mnatumia utaratibu wa kupima kwa kijiti. Huu hauna uhakika na huwezi kutegemea taarifa ya mtu mwingine au kuingia kwenye meli ya mtu na kuanza kuchukua vipimo hadi ujiridhishe. Nataka kujua ni kwa nini mlikuwa na utaratibu wa ku-bypass mafuta ili yasipite kwenye mita za kupimia mafuta? Ni kwa nini umetoa amri zianze kutengenezwa jana na siyo mwaka 2012 au 2013?” alihoji Waziri Mkuu.

Waziri Mkuu alisema mita hizo za Kurasini zilinunuliwa na Serikali kwa gharama za dola za marekani milioni 1.2 (wakati huo) na haiwezekani kuacha kuzitumia wakati watu wanachezea mifumo na kuongeza mianya ya kupoteza mapato kwa Serikali. Ameagiza mita hizo zianze kufanya kazi mara moja.

Wazir Mkuu alisema matumizi ya mita hizo yaliafikiwa na Serikali baada ya kubaini upotevu mkubwa wa kodi kwenye mafuta yanayoingizwa nchini na baada ya kuona hakuna tija ya kuendelea na ukadiriaji au kupokea taarifa za waagizaji peke yao.


Waziri Mkuu ambaye aliwasili Kurasini leo saaa 4: 30 asubuhi (Alhamisi, Februari 11, 2016) kwenye kitengo hicho kilichopo Kurasini (Kurasini Oil Jetty), alikagua mita hizo na kisha kwenda kukagua meli iliyokuwa ikishusha mafuta bila kutumia mita hiyo ya kupima mafuta yanayopokelewa kwa sababu mafundi walikuwa bado wanaendelea na ukarabati.

Akiwa Kurasini, Waziri Mkuu alielezwa na Bibi Chuwa kwamba mita hizo zilianza kufanyiwa ukarabati jana na leo asubuhi moja imekamilika ambayo ni ya kupokelea mafuta ya petroli. Ya dizeli ilikuwa inafunguliwa na mafundi na kukutwa imejaa kutu sababu ya kutotumika kwa muda mrefu.

“Hii ya dizeli imefunguliwa leo na ile ya mafuta ya kula, haijawahi kufanya kazi tangu ilipofungwa mwaka 2011,” alielezwa Waziri Mkuu na Kaimu Mkurugenzi wa Bandari, Eng. Aloyce Matei.

Alipoulizwa ni kwa nini aliamua kuzifungia mita hizo ziisifanye kazi, Bi. Chuwa alijibu kuwa alifikia uamuzi huo baada ya kupokea malalamiko kwamba zinawapunja wateja. Hata hivyo, hakufafanua ni wateja gani au wa aina gani.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu Majaliwa, ametembelea na kukagua mita mpya za kupimia mafuta ambazo zinajengwa Kigamboni. Mita hizo zimegharimu dola za marekani milioni 6 (sawa na sh. bilioni 12.96/- za sasa).

Akiwa hapo, Waziri Mkuu alielezwa kwamba ujenzi huo ambao ulianza miezi nane iliyopita, unatarajiwa kukamilika ifikapo katikati ya mwezi Machi, 2016. “Tunajitahidi kazi hii ikamilike ifikapo katikati ya mwezi ujao,” alisema Eng. John Bura, Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya BQ Contractors Ltd ambayo inasimamia ujenzi wa mita hizo.

Vilevile, Waziri Mkuu alitembelea sehemu ya kuchukulia mafuta yanayotoka bandarini (TPA Manfold) iliyoko Kigamboni na kukagua mitambo ya kusambazia mafuta kwenye matenki ya mafuta ya kampuni ya TIPER yaliyoko Kigamboni yanayomilikiwa kwa ubia bainaya Serikali na kampuni ya Oryx Energies.

Katika ziara hiyo ilibainika kuwa Kampuni ya TIPER imejiunganishia bomba la moja kwa moja kutoka kwenye bomba kubwa la mafuta linalotoka bandarini hali iliyomlazimu Waziri Mkuu kuagiza kwamba bomba hilo litolewe kwenye maungio hayo ndani ya mwezi mmoja.

“Natoa mwezi mmoja hili bomba liondolewe kwenye mfumo huu na kama yapo mabomba mengine pia yaondolewe,” alisema huku akionyesha karatasi iliyokuwa mfukoni kwake yenye mchoro unaobainisha kuwa kuna bomba jingine la inchi 10 limeungwa kinyemela kwenye bomba kuu.

“Kila mmoja anapaswa aje kuchukua pale kwenye manfold ili tujue nani kachukua nini. Msajili wa Hazina hili ni eneo lako na wewe unamiliki TIPER kwa asilimia 50, hebu simamia hili. Ninyi TPA leteni mapendekezo yenu Serikalini ili tuone tunaweza kudhibiti vipi vitendo kama hivi,” alisema Waziri Mkuu.

Pia alimtaka Msajili wa Hazina, Bw. Lawrence Mafuru awasiliane na Mwanasheria Mkuu ili waangalie upya mkataba na umiliki wa matenki hayo uwe chini ya Serikali kwa asilimia 100 ili mafuta yanayoagizwa na Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (Petroleum Bulk Procurement Agency) yaweze kuhifadhiwa huko.

Mapema, Waziri Mkuu ambaye alifuatana na Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Prof. Makame Mbarawa, alikagua eneo la manfold ya Mamlaka ya Bandari iliyopo Kigamboni na kukuta ni kampuni nne tu zenye matenki Kigamboni ambazo zinachukua mafuta yao hapo.

Kampuni hizo ni HASS, WORLD OIL, LAKE OIL na MOIL. TIPER haikutaka kufuata mfumo huo licha ya kuwa nafasi ya kufanya hivyo ipo. Kampuni nyingine zenye matenki yake nchi kavu, zinachukulia mafuta kwenye manfold ya Kurasini.

(mwisho)

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
2 MTAA WA MAGOGONI,

Tuesday, January 05, 2016

MAKATIBU WAKUU WAPYA OFISI YA WAZIRI MKUU WAANZA KAZI RASMI LEO




PICHA NO. 1
Katibu Mkuu Kilimo, Mifugo na Uvuvi Dkt. FlorenS Turuka ambaye awali alikuwa Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, (wa pili kulia) akisitiza jambo wakati makatibu wakuu wapya wa Ofisi ya Waziri Mkuu walipokutana na Menejimenti ya Ofisi hiyo (hawapo pichani) leo, tarehe 4 Januari, 2016, kulia kwake ni Katibu Mkuu (Bunge) Mussa Uledi, (wa kwanza kushoto) ni Katibu Mkuu (Kazi na Ajira) Erick Shitindi na (wapili kushoto) ni Katibu Mkuu (Sera) Dkt. Hamis Mwinyimvua.
(Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

PICHA NO.2
Baadhi ya wajumbe wa Menejimenti ya Ofisi ya Waziri Mkuu wakiwasikiliza makatibu wakuu wapya (hawapo pichani) wakati makatibu wakuu hao (hawapo pichani) walipokutana na Menejimenti hiyo leo, tarehe 4, 2016 Januari katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Jijini Dar es salaam.
(Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

PICHA NO.3
Katibu Mkuu (Kazi na Ajira), Erick Shitindi akisisitiza jambo wakati wa kikao na  Menejimenti ya Ofisi ya Waziri Mkuu (hawapo pichani) alipowasili katika Ofisi hiyo na makatibu wakuu wapya wengine wa Ofisi hiyo , leo, tarehe 4 Januari 2016,  (kulia kwake ) ni, Katibu Mkuu (Sera) Dkt. Hamis Mwinyimvua.
(Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

PICHA NO.4
Baadhi ya wajumbe wa Menejimenti ya Ofisi ya Waziri Mkuu wakiwasikiliza makatibu wakuu wapya (hawapo pichani) wakati makatibu wakuu hao (hawapo pichani) walipokutana na Menejimenti hiyo leo, tarehe 4 Januari, 2016 katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Jijini Dar es salaam.
(Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

PICHA NO.5
Baadhi ya wajumbe wa Menejimenti ya Ofisi ya Waziri Mkuu wakiwa na Makatibu wakuu wapya Katibu Mkuu, (Bunge) Mussa Uledi, (wa pili kushoto) pamoja na aliye kuwa Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo ambaye sasa ni Katibu Mkuu Kilimo, Mifugo na Uvuvi Dkt. FlorenS Turuka (wa tatu kutoka kushoto), Katibu Mkuu (Kazi na Ajira), Erick Shitindi (katikati) na Katibu Mkuu (Sera) Dkt. Hamis Mwinyimvua (watatu kutoka kulia) mara baada ya makatibu wakuu hao kukutana  na Menejimenti hiyo leo, tarehe 4 Januari, 2016. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

WAZIRI MKUU ATEMBELEA KIWANDA CHA TUMBAKU MKOANI RUVUMA NA KUWASIMAMISHA KAZI VIONGOZI WA CHAMA CHA USHIRIKA CHA SONAMCU



Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ametembelea kiwanda cha kusindika  tumbaku  cha mkoani Ruvuma na kuwasimamisha kazi viongozi wa Chama Cha Kikuu Cha Ushirika cha SONAMCU.

Akizungumza  jana jioni(Jumanne, Januari 5, 2016), katika ukumbi wa mikutano wa Ikulu Ndogo ya Songea, wakati alipokutana na wakulima wa zao la tumbaku wa Wilaya ya Namtumbo, Wananchama wa Vyama Vya Ushirika vya Mkoa wa Ruvuma, viongozi wa Mkoa pamoja na Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Edwin Ngonyani ambaye ni Mbunge wa Jimbo la Tunduru Kaskazini.

Waziri Mkuu amesema, Serikali ina dhamira ya kufufua kiwanda cha kusindika tumbaku cha SONAMCU, na lengo la kutembelea kiwanda hicho ni katika utekelezaji wa agizo la Rais John Pombe Magufuli la kufufua viwanda nchini.

Waziri Mkuu Majaliwa, ametembelea maeneno mbalimbali ya kiwanda hicho na kukagua mitambo iliyokua ikitumika kusindika tumbaku, kabla kiwanda hicho kuzimwa miaka kadhaa iliyopita  baada ya kukosa malighafi za kuendelea na uzalishaji.

Pia, amemtaka Afisa Biashara kutoka Wizara ya Viwanda na Biashara Bibi. Stela Lugongo kuandaa na kuwasilisha kwake mkakati wa kufufua kiwanda hicho cha kusindika tumbaku, na baadae kuwasimamisha kazi viongozi wote wa Chama Kikuu cha Ushirika cha SONAMCU waliohusika na tuhuma hizo na kutaka wafikishwe Mahakamani.

“Serikali imeazimia kufufua viwanda, hasa vile ambavyo havina wawekezaji vimebaki vyenyewe, Tunahitaji kujua namna ya kuvifufua”. Alisema Waziri Mkuu huku akishangiliwa.

Waziri Mkuu Majaliwa pia, amesikiliza  na kujibu kero mbalimbali za wakulima wa tumbaku wa Mkoa huo, ambao walilalamikia  mfumo wa Vyama vya Ushirika na namna ambavyo vyama hivi vimekua vikiwaibia fedha zao  hadi kushindwa kuendelea kulima zao la tumbaku na kukosa masoko ya mazao yao.

Aidha, Waziri Mkuu amewasihi wakulima kuwa watulivu na kusubiri maamuzi ya Mahakama baada ya kuwa viongozi wa Chama cha Ushirika SONAMCU ambao wamehusika na wizi wa fedha za wakulima kiashi cha Shilingi milioni 800 kwa kipindi cha mwaka 2011 hadi 2014 tayari wamefikishwa Mahakamani na uchunguzi unaendelea. Pia, amemwagiza Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Said Thabit Mwambungu kukutana na wakulima hao ili kupatia ufumbuzi matatizo yao.

Aidha, ametoa wito kwa wakulima kuendelea kulima zao la tumbaku kwa kuwa linaongeza pato la mtu mmoja mmoja, linasaidia kuchangia pato la Mkoa na kukua kwa uchumi wa nchi. Amewashauri wakulima kuunda  na kuviendesha Vyama Vya Ushirika kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizopo.

Waziri Mkuu amemaliza ziara yake mkoani Ruvuma, atafanya majumuisho ya ziara hiyo leo, kabla ya kuagana na viongozi wa Chama na Serikali na kurejea jijini Dar es Salaam.

(mwisho)

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU

WAZIRI MKUU AKAGUA JENGO LA MAKAO MAKUU YA HALMASHAURI YA WILAYA YA SONGEA


Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amekagua jengo la Makao Makuu ya Halmashauri ya Wialaya ya Songea lilipo katika kijiji cha Lundusi, Wilaya ya Peramiho mkoani Ruvuma.

Alipowasili  jana katika eneo hilo alikutana na viongozi wa jadi ambapo  Mzee Daniel Gama  alimkabidhi  ngao na silaha ikiwa ni ishara ya kumkaribisha kijijini hapo, pia alipata fursa ya kutazama ngoma ya mila ya kabila la Wangoni.

Mara baada ya kukagua jengo hilo  la ghorofa,Mkurugenzi wa Halmashauri ya Lundusi Bwana Rajabu Mtiula amesema jengo hilo lenye  ofisi 50, vyoo 4, ukumbi mkubwa 1 na kumbi ndogo 2, ambapo mradi huo umetekelezwa kwa fedha za mfuko wa Mradi wa Maendeleo na Serikali. Hadi sasa Serikali imetoa kiasi cha zaidi ya  shilingi bilioni 200 na utekelezaji wake umekamika kwa 85%, hivyo wanatarajia kuanza kutumia jengo hilo mwezi Februari, 2016.

Akizungumza  jana  (Jumatatu, Januari 4, 2016)  na wananchi wa kijiji cha Lundusi, Waziri Mkuu, amewapongeza   wananchi  wa Lundusi kwa hatua hiyo ya maendeleo na kusema kuwa Serikali itaendelea kuunga mkono ujenzi wa jengo hilo.

Waziri Mkuu Majaliwa, ametaka kuwepo na mikakati ya uboreshaji wa eneo hilo kwa kusogeza huduma karibu ili kuvutia watu zaidi katika eneo hilo.

Naye, Waziri wa Nchi  Ofisi ya Waziri Mkuu, Bunge, Sera, Uratibu, Ajira na Walemavu  Jenista Mhagama  ametoa pongezi kwa Mheshimiwa Rais Dkt. John Magufuli na Waziri Mkuu kwa kuchaguliwa na kuongoza Serikali ya Awamu ya Tano.

Pia, ameishukuru Serikali kwa kusaidia kujenga jengo hilo, na pia ameeleza kero mbalimbali zinazowakabili wananchi wa maeneo hayo ikiwemo wakulima kutofaidika kwa bei ya soko ya kuuza mahindi, kutokuwepo na umeme na maji.

Aidha, Waziri Mkuu Majaliwa alimuagiza Waziri Jenista kufuatilia kero hizo kwa Wizara husika na baadae kuleta mrejesho kwa wananchi.

Waziri Mkuu Majaliwa anaendelea na ziara mkoani Ruvuma, leo siku ya jumanne (Januari 5, 2016)  atatembelea na kukagua Hospitali ya Rufaa ya Mkoa na kuongea na Watumishi wa hospitali hiyo  na baadae ataongea na Watumishi wa Umma.

(mwisho)

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU

WAZIRI MKUU AKAGUA MAGHALA YA WAKALA WA HIFADHI YA TAIFA YA CHAKULA (NFRA) KANDA YA SONGEA


Waziri Mkuu  Kassim  Majaliwa amekagua  maghala ya Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) kanda ya Songea, wakati akiendelea na ziara yake mkoani Ruvuma.

Akizungumza na wafanyakazi wa Wakala hiyo, wadau wa kilimo pamoja na wananchi jana, (Jumatatu, Januari 4, 2016) nje ya majengo ya Wakala mara baada ya kukagua mahindi yaliyohifadhiwa katika maghala  ya Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) kanda ya Songea , mkoani Ruvuma amesema  kufuatia taarifa ya kuwepo na baadhi ya maeneo yenye njaa nchini, Serikali imetoa tamko kuwa hakuna mtanzania atayakekufa kwa njaa.

Ambapo, Serikali  kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu kitengo cha Maafa imeweka mikakati ya  kukabiliana na  tatizo la  njaa kwa kutoa msaada wa chakula katika maeneo yanayokabiliwa na njaa.

 “Ni wajibu wangu kuhakikisha nasimamia vizuri hili, nimeona hali ya uhifadhi  wa chakula, tunayo mahindi ya kutosha lakini hakuna sehemu ya kuhifadhi chakula” amesema Waziri Mkuu.

Waziri Mkuu Majaliwa ameendelea kwa kusema uwezo wa maghala hayo yaliyopo chini ya Wakala Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) kanda ya Songea yana uwezo wa kuhifadhi tani 29 pekee   na Songea  inauwezo wa kuzalisha zaidi tani 70 hadi 80.

Pia , ameagiza  Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) kanda ya Songea , kuanzia mwaka huu kwa kushirikiana na Wakuu wa Mikoa pamoja Wakuu wa Wilaya  kuanzisha  vituo vya kununulia mahindi  na kuhakikisha magunia yanawafikia wakulima katika vituo hivyo ambapo wataweza kuhifadhi mahindi  na  kuuza  kwa bei ya kwenye soko.

Waziri Mkuu  pia, ameitaka Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) kanda ya Songea ,kutumia teknolojia ya kisasa ya uhifadhi wa chakula, kuandaa utaratibu maalum utakaozuia msongamano wa  malori  yanayosubiri kupata huduma ya kununua mahindi  nje ya majengo ya Wakala na kukamilisha miradi itakayosaidia Wakala kuwa na fedha za kutekeleza majukumu yake.

Kwa upande wake, Meneja Hifadhi wa  Chakula kanda ya Songea, Bwana. Morgan Mwaipaya amesema kati ya maghala 33 ya kuhifadhi mahindi nchi nzima, Songea ina maghala 6 kati ya hayo. Hivyo, Wakala imeweka vipaumbele vyake ambavyo ni  pamoja na kutoa chakula cha msaada kwa maeneo yenye matatizo ya njaa, kuongeza upatikanaji wa mahindi ili kuzuia kupanda kwa bei ya chakula mwaka 2015 – 2016, Wakala kununua na kuhifadhi  mahindi katika maeneo yaliyozalisha zaidi na kuzingatia sehemu ya sehemu ya akiba ya chakula na kuuza kwa wakulima, mawakala pamoja na Wakala wa Chakula duniani (World food program).

Amesema Wakala imeandaa mikakati ya mbalimbali ikiwemo  kuongeza  uwezo  wa tani 24600 hadi tani  45000 kwa mwaka 2014- 2017, kuboresha mfumo wa utendaji kazi kwa kutumia mifumo ya stahili ya TEHAMA na kutumia fursa za mikopo kutoka Taasisi mbalimbali za kifedha ili kuendesha shughuli za uwezeshaji I kiwemo kuelimisha taratibu za ununuzi kwa mawakala.

Naye, Mbunge wa Jimbo la Songea, Mheshimiwa Leonidas Gama amesema   wakulima wachache wamekua wakiuza mahindi yao kwa bei ya soko,  wengi wao wamekua wakiuza mahindi kwa mawakala kwa bei ya shilingi 150 hadi 200  kwa kilo na  wakala wakiuza kwa shilingi 500 kwa Serikali. Ambapo amemuomba  Waziri Mkuu  kutatua tatizo la soko la mahindi kwa wakulima. Hata hivyo Waziri Mkuu ametoa wito kwa wakulima kuendelea kuzalisha mahindi akiahidi Serikali kununua mahindi hayo kwa bei ya soko  ambayo itamnufaisha mkulima.

Waziri Mkuu Majaliwa anaendelea na ziara mkoani Ruvuma, leo siku ya jumanne(Januari 5, 2016)  atatembelea na kukagua Hospitali ya Rufaa ya Mkoa na kuongea na Watumishi wa hospitali hiyo  na baadae ataongea na Watumishi wa Umma.

(mwisho)

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,