Wednesday, January 29, 2014

WAZIRI MKUU ATAKA WAKAZI PUGU WAJIUNGE KWENYE SACCOS


*Azindua kisima cha maji, awapigia debe kwenye umeme
*Amtaka RC Dar azuie michango ya darasa la kwanza

WAZIRI MKUU Mizengo Pinda amewataka wakazi wa Dunda ‘A’ na Dunda ‘B’ wajiunge kwenye Vyama vya Kuweka na Kukopa (SACCOS) na wavisajili kwenye Halmashauri yao ili waweze kukubalika kupatiwa mikopo.

Alikuwa akizungumza na wakazi wa eneo hilo jana jioni (Jumanne, Januari 28, 2014), lililopo Mtaa wa Kigogo Fresh Kata ya Pugu wilaya ya Ilala nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam kwenye hafla fupi ya uzunduzi wa kisima cha maji kwa ajili ya wakazi wa eneo hilo.

Waziri Mkuu aliwataka wasajili vyama vyao ili waweze kutambulika kwa urahisi na waweze kuwa na watu wenye dhamana ya kurejesha mikopo mara watakapoanza shughuli za ujasiriamali.

“Tatizo letu ni ukosefu wa anuani za makazi ili wakopaji watambulike na waweze kurejesha mikopo. Tunasisitiza SACCOS kwa sababu tunajua kutakuwa na watu wenye dhamana ya kusimamia urejeshwaji wa mikopo hii,” alisema wakati akijibu swali la Bw. Abdallah Mwaking’inda na wakazi wa Dunda.

Vilevile, alitumia fursa hiyo kumwagiza Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Bw. Said Meck Sadick afuatilie shule ambazo zinatoza michango kwa watoto waliopaswa kuandikishwa darasa la kwanza lakini wakashindwa kuazna shule kwa sababu ya michango hiyo.

“Uandikishwaji wa watoto wanaoanza darasa la kwanza ni wa lazima kwa kila mtoto, tulifanya hivyo ili tuhakikishe watoto wote wapate elimu. Sasa kama mzazi ana watoto wawili au watatu akishindwa kuwalipia manake watoto hao wamebaki nyumbani,” alisema.

“RC litazame vizuri suala hili kwa sababu kama zoezi la uandikishaji ni hili, ina maana kuna wazazi watashindwa kuwapeleka watoto shule,” alisema.

Mapema, kwenye risala yao, wakazi hao wa Dunda ‘B’ walimshukuru Waziri Mkuu kwa kuwaunganisha na mfadhili kutoka taasisi ya REHEMA ambayo imewajengea kisima hicho chenye urefu wa mita 90, tenki la lita 10,000 na mnara wa mita 20 wa kuwekea tenki hilo kwa gharama ya sh. milioni 20.

Walimuomba pia Waziri Mkuu awasaidie kupata umeme wa three phase ili uweze kutosheleza mahitaji ya eneo zima la Dunda ikiwa ni pamoja na kuendesha kisima chao.

Akijibu haoja hiyo, Mhandisi Theodori Bayona kutoka TANESCO makao makuu alisema watarudisha huduma ya three phase iliyokuwepo zamani lakini ikaondolewa kwa sababu ya wizi wa mara kwa mara. Aliwaomba wakazi hao wawe walinzi wa nyaya pindi watakapowekewa na kwamba watatakiwa kulipia service line ya kawaida ili umeme upelekwe hadi kisimani moja kwa moja.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Bw. Said Meck Sadick aliwahidi kuwachangia tenki moja la lita 10,000 ili waweze kuwa na ujazo mkubwa wa maji kwenye matenki yao na kuepusha kazi ya kupampu maji mara kwa mara.

Kwa mujibu wa mkuu huyo wa mkoa, wenye magari yanayobeba maji, wanauza ndoo moja kwa sh. 400/- katika eneo hilo.

(mwisho)

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
S. L. P. 3021,
DAR ES SALAAM.

Tuesday, January 28, 2014

MAMBO YA CHAKULA CHA MCHANA KILICHOANDALIWA NA SHIRIKA LA MASISTA WA CANOSSA KWA WATOTO WAISHIO KATIKA MAZINGIRA MAGUMU

Mkuu wa mkoa wa Kagera Kanali Mstaafu Fabian Massawe akiangalia kwa makini watoto waishio katika mazingira magumu aliposhiriki nao pamoja kwenye chakula cha mchana kilichoandaliwa na shirika ma masista wa CANOSSA lililoko mkoani Kagera.

TAMKO LA JUMUIYA YA VIJANA KUUNGA MKONO KAZI YA SEKRETARIETI YA CHAMA CHA MAPINDUZI CHINI YA KATIBU MKUU NDUGU ABDULRAHAMAN KINANA



“Inapofikia wasimamizi wa Kanuni za Chama wanapigwa vita ya wazi kwa uamuzi wao wa kukisimamia Chama, tafsir yake ni moja tu watu wanaowapiga vita hawakitakii mema chama chetu.”

“..Chama Cha Siasa chochote  duniani hubomoka kutokana na migongano iliyokithiri ya muda mrefu. Uzoefu wa vyama vikubwa vilivyoporomoka umeonyesha hivyo!  Chama lazima kidhibiti uchu wa madaraka wa baadhi ya viongozi wake na ndani ya serikali yake...” – Dr Eginald P. Mihanjo

“..Chama cha siasa ni itikadi. Chama cha siasa ni siasa kwa maana halisi ya neno lenyewe siasa –“siasa”. Ni mahali ambapo watu wenye madhumuni mamoja yaliyoainishwa waziwazi hukutana na kuwa kitu kimoja.  Chama cha siasa sio mkusanyiko wa “majini dume yenye tamaa”, - majini ambayo yametanguliza mbele tamaa kufa na kupona-tamaa ya kutengeneza pesa au kupata vyeo kwa gharama   yoyote! – Dr Bashir Ally


UTANGULIZI:

Hili ni tamko la vijana makini wa jumuiya ya umoja wa vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) kuunga mkono juhudi na utendaji wa sekretarieti ya halmashauri kuu ya Chama Cha Mapinduzi ikiongozwa na Katibu Mkuu Komredi Abdulrahaman Kinana.
Maneno ya utangulizi yamebeba dhima ya tamko hili, kufuatia taarifa zilizoripotiwa kwenye baadhi ya vyombo vya habari vikiwanukuu baadhi ya wanachama wa Chama Cha Mapinduzi,wakiwatuhumu Viongozi wa Sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya CCM, Katibu Mkuu Ndugu Abdulrahaman Kinana na Katibu wa Itikadi na Uenezi  Ndugu Nape Moses  Nnauye.
Sisi Vijana tunatambua kuwa tuhuma hizo na maneno hayo ya hovyo yametolewa kwa nia ovu yenye kulenga kuwakatisha tamaa Viongozi hao wa Chama. Tunafahamu kuwa upo mkakati wa kiuhaini ulioandaliwa na kuratibiwa na “mtandao” ndani ya Chama ambao umejipanga kuendesha uhaini huo.
Sisi vijana wa UVCCM tunatambua na kuthamini juhudi za Katibu Mkuu na Sekretarieti yake katika kukijenga na kukiimarisha Chama kwa kuisimamia barabara misingi na shabaha ya kuundwa kwake, katika umri wetu hatukuwahi kuona Chama kikiwa karibu na wananchi kwa kufuatilia, kusikiliza na kushiriki katika utatuzi wa kero, shida na changamoto zao kama ilivyo katika kipindi hiki chini ya Comrade Kinana na timu yake. Juhudi hizi ni za kuungwa mkono na kamwe si za kubezwa na mwanaCCM muadilifu, muaminifu na mwenye mapenzi ya kweli kwa Chama.
Juhudi za kukiimarisha Chama kutoka ngazi za chini, kwa mabalozi ni mkakati bora kuwahi kutekelezwa na Chama, kukirudisha Chama kwa wanachama ni kutimiza lengo la kuundwa kwa Chama hiki, Chama hiki ni cha wanyonge, masikini wa Taifa hili, HAIWEZEKANI matajiri watake kukihodhi na waratibu mikakati ya kukihujumu kwa pesa zao hali sisi vijana tukitazama, tunasema tutakilinda Chama chetu na tutawalinda viongozi wetu waadilifu.
Ni hawa ambao wanabezwa leo ndio wameweza kurudisha Imani ya wananchi kwa Chama, Imani na matumaini ambayo tayari yalishaanza kupotea na Chama kuonekana si tena cha wanyonge, wakulima na wafanyakazi wa nchi hii.
Ni Comrade Kinana na timu yake ndio waliozunguka kwenda kukutana na wakulima wa Pamba kule mikoa ya Kanda ya ziwa na kumpeleka balozi wa China na kumshawishi kujenga viwanda ili kuboresha manufaa kwa wakulima.
Ni Comrade Kinana na timu yake ndio waliokwenda Kusini kukutana na wakulima wa Korosho na kushirikiana nao pamoja na bodi kutatua tatizo la Korosho.
Ni Comrade Kinana na timu yake ndio walioibua hoja na kero za wafugaji, walimu na wananchi kwa ujumla, na kuwataka viongozi wa Serikali kuhakikisha wanawajibika kwa wananchi walipa kodi wa Taifa hili.
Kupinga mafanikio ya Ziara hizo ni kupinga utetezi wa wanyonge.
Mtu anayebeza ziara hizo na kuwaita Viongozi waliozifanya waropokaji na wahuni wahuni ni mtu mjinga, mtu wa hovyo,hana maadili, asiyekipenda Chama, mhaini na mzandiki anayepaswa kuchukuliwa hatua kali za kinidhamu ili iwe fundisho kwa wengine.
TAMKO hili limezingatia wosia wa Baba wa Taifa, muasisi wa Chama Cha Mapinduzi Mwl Julius Kambarage Nyerere katika kitabu Chake TUJISAHIHISHE.

Imetolewa na Paul Makonda.
Katibu wa Hamasa na Chipukizi. 

Monday, January 27, 2014

RAIS - RICKETTS - TABULETI

 Rais Jakaya Mrisho Kikwete akipokea  akipokea moja ya Tabuleti 61  kwa ajili ya wanafunzi wa kidato cha pili katika Shule ya Wama Nakayama iliyoko kijijini Nyamisati, Rufiji, Mkoa wa Pwani    toka kwa Mwenyekiti wa taasisi ya kusaidia elimu ya Opportunity Education Foundation wa Marekani Bw. Joe Ricketts wakati alipomtembelea Ikulu Jumapili Januari 27, 2014

 Mwenyekiti wa taasisi ya Wanawake na Maendeleo (WAMA) Mama Salma Kikwete, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi Dkt Shukuru Kawambwa, Mwenyekiti wa Bodi ya Shule ya WAMA Nakayama Dkt Ramadhani Dau na Mkuu wa Shule hiyo wakipokea moja ya Tabuleti 61 alizozitoa kwa ajili ya wanafunzi wa kidato cha pili katika Shule ya Wama Nakayama iliyoko kijijini Nyamisati, Rufiji, Mkoa wa Pwani leo Januari 27, 2014 toka kwa  Mwenyekiti wa taasisi ya kusaidia elimu ya Opportunity Education Foundation wa Marekani Bw. Joe Ricketts akikabidhi moja ya Tabuleti 61 alizozitoa kwa ajili ya wanafunzi wa kidato cha pili katika Shule hiyo.


Serikali kusambaza tabuleti za kufundishia sekondari

Yaanza kazi hiyo kwa kushirikiana na taasisi ya Marekani ya Opportunity Education Trust
Serikali inakusudia kutoa maelfu kwa maelfu ya tabuleti za kufundishia masomo mbali mbali  kwa wanafunzi na walimu wa shule za sekondari nchini kama njia ya ubunifu zaidi, ya kisayansi na ya uhakika ya kukabiliana na changamoto zinazoikabili sekta ya elimu kwa kutumia Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (ICT).

Ili kufanikisha mpango huo, Serikali inakusudia kuingia ushirikiano (partnership) na taasisi isiyokuwa ya kiserikali ya Opportunity Education Trust ya Marekani ambayo leo, Jumatatu, Januari 27, 2014, inazindua mpango wa majaribio wa utoaji wa tabuleti hizo kwa wanafunzi na walimu wao wa shule za sekondari nchini.

Mpango wa Serikali wa kusambaza tabuleti kwa wanafunzi na walimu wa shule za sekondari ulitangazwa usiku wa jana, Jumapili, Januari 26, 2013 na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete wakati alipokutana na kuzungumza na Bwana Joe Ricketts, mwenye taasisi ya Opportunity Education Trust na mmoja wa matajiri wa Marekani.

Katika mazungumzo hayo yaliyofanyika Ikulu, Dar es Salaam, Rais Kikwete amemweleza kwa undani Bwana Ricketts hatua ambazo zimechukuliwa na Serikali yake kupania na kuboresha elimu tokea mwaka 2006, hatua ambazo zimechangia kupanua kwa kasi na kwa kiwango kikubwa wigo wa utoaji elimu nchini na changamoto ambazo zimezuka kutokana na upanuzi huo mkubwa.

Rais Kikwete amesema baadhi ya changamoto hizi ni ukosefu wa walimu, na hasa walimu wa masomo ya sayansi, na ukosefu wa vitabu vya kufundishia changamoto mbili kubwa ambazo zinatatuliwa na matumizi ya tabuleti.

“Mbali na upanuzi mkubwa wa nafasi za wanafunzi kupata elimu ya ngazi mbali mbali, pia tumepanua sana ufundishaji wa walimu. Mwaka 2005, vyuo vyetu vyote vilikuwa vinatoa walimu 500 sasa tunatoa walimu 12,000 kwa mwaka. Hivyo, tunaamini kuwa katika mwaka mmoja ama miwili ijayo, tutakuwa tumemaliza tatizo la walimu wa masomo ya sanaa,” Rais Kikwete alimwambia Ricketts na kuongeza:

“Lakini bado tunakabiliwa na upungufu mkubwa wa walimu wa sayansi, kama zilivyo nchi nyingine. Tuna upungufu wa walimu 26,000 na kwa mwaka vyuo vyetu vyote vinahitimisha walimu 2,100 tu. Hii ina maana kuwa itabidi kusubiri miaka 13 kuweza kumaliza tatizo hili kwa mahitaji ya sasa. Hili haliwezekani na hii ndiyo maana halisi ya kutumia sayansi na teknolojia ya namna hii kufundishia wanafunzi wetu.”

Rais Kikwete alisema kuwa matumizi ya teknolojia kufundishia nchini ni jambo linalowezekana kwa urahisi kwa sababu mtandao wa mawasiliano wa National Fibre Network ambao karibu umefikia kila wilaya sasa.

Rais Kikwete alimshukuru Bwana Ricketts na  taasisi yake kwa kukubali kuchangia maendeleo ya sekta ya elimu nchini kwa kusambaza teknolojia ya kisasa kama moja ya njia za ubunifu zaidi za kufundishia hasa masomo ya sayansi.

Chini ya mpango huo wa majaribio wa kusambaza teknolojia hiyo ya kisasa, taasisi ya Opportunity Education Trust inatoa tabuleti 1100 kwa ajili ya walimu na wanafunzi wa sekondari katika shule 33.

Bwana Ricketts ambaye ni mwenyeji wa Omaha, Nebraska alimwambia Rais Kikwete: “Hapa tunafanya majaribio na Tanzania ni nchi ya kwanza duniani miongoni mwa nchi ambazo tunaunga mkono mipango ya maendeleo kunufaika na mpango huo wa majaribio. Ni azma yetu kuwa baada ya kuwa tumefanya tathmini ya mafanikio na changamoto za hatua hii ya majaribio, tutaupanua mpango huu kushirikisha shule nyingi zaidi kwa kushirikiana na Serikali kwenye mpango wake mkubwa wa kusambaza teknolojia hii katika shule zote za sekondari hapa Tanzania.”

Bwana Ricketts na wataalam wake pamoja na maofisa wa Serikali wameanza kutekeleza mpango huo leo, Jumatatu, Januari 27, 2014, kwa kutoa tabuleti kwa wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Wama Nakayama iliyoko Mkoa wa Pwani.

Baada ya leo, shughuli hiyo itahamia Zanzibar na Pemba, kabla ya Bwana Ricketts na wataalam wake kutoa tabuleti kwa shule zilizoko mikoa ya Arusha, Dar es Salaam, Dodoma, Mwanza, Kagera na Morogoro.

Shule zinazonufaika katika mpango huo ni za Serikali na binafsi na kwa kuanzia masomo ambayo yanapatikana katika tabuleti hizo ni hesabu, jiografia, historia na kiingereza.

Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu,
DAR ES SALAAM.

Sunday, January 26, 2014

CHADEMA YAITIKISA BUKOBA

 Mwenyekiti wa CHADEMA taifa Freeman Mbowe akitafakari jambo kabla ya kuwahutubia maelfu ya wananchi wa mji wa bukoba waliojitokeza kumsikiliza leo kwenye uwanja wa mashujaa ulioko katika manispaa ya Bukoba.
 Mbunge wa jimbo la ubungo, Mnyika akiwa na mkurugenzi wa idara ya usalama ya CHADEMA, Willfred Lwakatare ambaye ni mwiba wa mbunge wa jimbo la Bukoba mjini, aliyejiuzulu uwaziri wa maliasili na utalii baada ya kukumbwa na kafsha Balozi Khamis Kagasheki.
Baadhi ya wananchi katika manispaa ya Bukoba.









Thursday, January 23, 2014

BALOZI KAGASHEKI AWASILI BUKOBA AAHIDI KULA SAHANI MOJA NA MEYA AMANI ASIYEPENDA KUTEKELEZA AGIZO LA WAZIRI MKUU MIZENGO PINDA LA KUMTAKA AACHIE NGAZI

Mwenyekiti wa CCM wa wilaya ya Bukoba mjini akiratibu mkutano wa mbunge wa jimbo la Bukoba mjini Balozi Sued Kagasheki uliofanyika kwenye uwanja wa Bukoba.
Balozi Kagasheki akipongezwa alipofika kwa mara ya kwanza jimboni baada ya kujiuzulu wadhifa wake wa nafasi ya uwaziri wa maliasili na utalii.
Mjumbe wa NEC CCM wa wilaya ya Bukoba, Abdul Kagasheki naye hakubaki nyuma.
Baadhi ya wananchi waliojitoikeza kumpokea.
Balozi Kagasheki akiongea na wananchi wa jimbo la Bukoba mjini, katika hotuba yake amesisitiza kuwa Meya Amani sio Meya kama anavyotangaza kupitia kwenye vyombo vya habari kuwa hakubaliani na taarifa wa mkaguzi na mdhibiti wa hesabu za serikali, anasema kama anasema hajajiuzulu atakumbana na kura za kutokuwa na imani naye, amemtaja Meya Anatory Amani kuwa ni ndiye chanzo cha kudumaza maendeleo katika manispaa ya Bukoba, anasema kiasi cha bilioni zaidi ya 2 ambazo amezitumia bila maelezo kuwa zingefanya shughuli nyingi za kuwaletea maendeleo wananchi.
Baadhi ya viongozi wa CCM walioudhuria mkutano uliandaliwa na Balozi Kagasheki.

RAIS KIKWETE NCHINI USWIS

Rais Jakaya Kikwete akihutubia wakati wa mkutano wa kujadili namna ya kuongeza kasi  ya uboreshaji wa kilimo uliofanyika  Davos Uswis.
 Rais Jakaya Kikwete akishangiliwa baada ya kuhutubia wakati wa mkutano wa kujadili namna ya kuongeza kasi  ya uboreshaji wa kupatikana na kulinda maji nsalama kwa miaka ijayo  katika hoteli ya Derby huku  Davos  Uswisi.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akutana na kufanya mazungumzo na Mkuu wa Shirika la Maendeleo ya Kimataifa ya Marekani (USAID) Mhe Rajiv Shah katika ukumbi wa mikutano wa Davos, Uswisi,
Rais Jakaya Mrisho Kiwete kutana na kufanya mazungumzo na  Mwenyekiti na Mtendaji Mkuu wa kampuni ya JETRO ya Japan katika hoteli ta Sheraton Davos,  Uswisi.

Tikitaka za Mzee Reginald Mengi: Anamiliki share katika makampuni yenye vitalu vya mafuta na gesi.



Katika Mjadala uliofungwa hivi karibuni na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dr Jakaya Mrisho Kikwete juu ya suala la Uzawa kwenye utafutaji na uzalishaji wa mafuta na gesi hapa nchini. Mjadala huo ambao kwa kiasi kikubwa ulibebwa na pande mbili yaani upande wa Serikali chini ya Waziri wa Nishati na Madini Mheshimiwa Prof Sospeter Muhongo na upande wa sekta binafsi chini Mzee Reginald Mengi. Tamati ya Mjadala huo ambapo Rais Jakaya Kikwete aliufunga kwa kubainisha kuwa inatosha kwa makampuni ya Serikali kuwawakilisha watanzania katika mchakato wa ushirikishwaji wao katika utafutaji na uvunaji kwa kuwa gharama za mchakato huo ni wa gharama kubwa ambao watanzania wazalendo walio wengi hawana uwezo wa kumudu.

Hitimisho hilo ambalo limekuwa mwiba kwa Mwenyekiti wa Sekta Bnafsi Nchini Bwana Reginald Mengi kwa kuwa si tu ni kiongozi wa sekta binafsi nchini bali pia ni mtu mwenye maslahi ya moja kwa moja na biashara ya utafutaji, uchimbaji na uvunaji wa rasilimali za madini, mafuta na gesi. Hitimisho hilo ni mwiba kwa kuwa hoja aliyoisimamia imeonekana kushindwa mbele ya jamhuri.

Lakini taarifa iliyopatikana punde ambayo ni sahihi, na ambayo imeendelea kuonyesha sarakasi za Mzee Mengi katika suala hilo ni kwamba; Mzee Mengi ni mbia mwenye shares kwa asilimia 3.3 katika kampuni ya watanzania inayofahamika kwa Jina la SWALA ambayo ina blocks 2 za kutafuta mafuta na gesi huko Kilombero  na Pangani. Kampuni hiyo ambayo inaongozwa na Mwenyekiti wa Bodi Bwana E. Massawe na Mkurugenzi wake Bwana B Mramba.

Taarifa hizi zinaudhihirishia Umma kuwa Mzee Mengi anapigania hoja hii kwa maslahi binafsi na pili inaonyesha ni kwa namna gani amekuwa ni mtu asiyeridhika pamoja na kumiliki sehemu kubwa ya ardhi yenye madini na hata kufanikiwa kupata nafasi katika vitalu vya gesi na mafuta ameendelea kumshutumu Waziri wa Nishati na Madini kwa tuhuma za kutengeneza na hata kumkashifu kuwa ni kiongozi wa Hovyo ambaye anafaa kupelekwa milembe kuangaliwa akili yake.

Kwanza ni makosa na kinyume cha Sheria na Kanuni za Madini kwa mtu mmoja kujilimbikizia eneo kiasi hicho, na makosa mengine ni kuwa yapo maeneo ambayo hajayaendeleza na sheria inaweka bayana kuwa baada ya miaka 2 mtu asiyeendeleza eneo lake anatakiwa kunyang'anywa asilimia 50 ya eneo hilo, na usipoliendeleza lililobaki  katika miaka 2 ijayo unapoteza eneo zima, hivyo kwa maeneo ambayo Mzee Mengi anayamiliki na hajayaendeleza ni vyema sheria ikafuata mkondo wake na anyang'anywe maeneo hayo.


Kauli za Mzee Mengi na mtindo wa Shutuma zake kwa Waziri ulionesha ni kwa kiasi gani Mzee Huyu amekosa busara na hekima katika kufuatilia na kufikisha hoja zake, lakini utumiaji wa vyombo vya habari anavovimiliki na vile ambavyo ana ushawishi navyo kuwashutumu mahasimu wake na hata kuwakatisha tamaa watanzania juu ya mipango na mikakati ya maendeleo ya Serikali yao ni makosa mengine ya msingi katika tasnia ya habari na kwake kama mmiliki, makosa ambayo ni ya kukusudia na yenye kutoa taswira mbaya mbele ya jamii.

Umefika wakati wa watanzania kuwaelewa watu hawa ambao katika macho ya jamii wanajipambanua kama wapigania haki, wakweli na wenye huruma hali ya kuwa uhalisia wa ndani ni watu wabadhirifu, walafi na walanguzi wasiotosheka.

Wednesday, January 22, 2014

Kashfa ya kasisi kujipa 'fedha chafu'


Kasisi Monsignor Nunzio Scarano
Kasisi mmoja mkuu nchini Italia, amefikishwa mahakamani kwa kosa la kuhaulisha mamilioni ya dola au kujipatia pesa kwa njia haramu, kupitia kwa benki ya Vatican.
Polisi wanasema kuwa Monsignor Nunzio Scarano, anakabiliwa na kosa lengine la kupanga njama ya kuingiza kiharamu dola milioni 26 nchini Italia na kwamba yuko chini ya kifungo cha nyumbani.
Mhasibu huyo wa zamani wa Vatican na watu wengine wawili, walipokea kibali cha kukamatwa siku ya Jumanne.
Mwaka jana Papa Papa Francis aliunda tume, ya kutathmini shughuli za kanisa hilo baada ya kashfa kadhaa kujitokeza kuhusu kanisa hilo.
Vatican imekataa ombi la idara ya mahakama ya Italia kuchunguza madai hayo, yaliyotendwa na maafisa hao kwa misingi ya kidiplomasia.
Lakini chini ya uongozi wa Papa Francis, ushirikiano umeimarika kati ya Maafisa wa Italia na Vatizan ambao ulipelekea kukamatwa kwa Kasisi Monsignor Scarano, majira ya joto.
Mnamo Jumanne polisi walipata Euro milioni 6.5 katika akaunti ya benki pamoja na katika nyumba ya Kasisi Monsignor Scarano mjini Salerno.
Maafisa wakuu wanasema kwamba mashitaka ya sasa hivi dhidi ya Monsignor Scarano ni kuhusu kutoa michango bandia ambayo inasemekana ilitoka katika benki zingine kimataifa.