Friday, September 06, 2013

KIKWETE ATAJA SIFA ZA KIONGOZI BORA


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amesema kuwa kazi kuu na kipimo halisi cha kiongozi bora na hodari ni jinsi kiongozi anavyohangaikia maendeleo ya wananchi, ubunifu wake wa kuwaongezea wananchi mapato na kujali kumaliza kero zao.
Aidha, Rais Kikwete amesema kuwa kazi ya madiwani nchini haiwezi kuwa ni kupokea posho za vikao ama kupima na kujigawia viwanja bali iwe ni kupambana na umasikini wa wananchi ambayo ndiyo kazi waliyoomba wakati wanatafuta kura za kuwa madiwani.
Vile vile, Rais amewataka madiwani wote nchini kutumia haraka na ipasavyo fedha zinazotolewa kwa ajili ya ujenzi wa barabara ndani ya halmashauri zao na siyo kuziweka hadi mwisho wa mwaka wa fedha na kulazimika kuzirudisha kwenye Mfuko wa Barabara.
Rais Kikwete ameyasema hayo leo, Ijumaa, Septemba 6, 2013, wakati alipopokea Taarifa ya Maendeleo ya Wilaya ya Misungwi wakati alipoanza ziara ya siku tano katika Mkoa wa Mwanza kukagua na kufungua shughuli na miradi ya maendeleo.
                                         Akiuliza maswali na kutoa maelekezo wakati Ripoti hiyo inawakilishwa na Mkuu wa Wilaya ya Misungwi, Bibi Mariam Lugaija kwenye Shule ya Sekondari ya Misungwi, Rais Kikwete amewaambia viongozi wa Wilaya hiyo na wa Mkoa wa Mwanza:
“Kazi muhimu na uhodari wa kiongozi unathibitishwa na jinsi kiongozi huyo anavyopambana kupunguza umasikini wa wananchi na anavyobuni mbinu za kuongeza mapato ya wale anaowaongoza.”
Ameongeza Rais Kikwete: “Kila kiongozi lazima awe na uchungu wa maendeleo na tamaa ya kuleta mabadiliko kwa wananchi wao. Kazi ya kiongozi ni kuhangaika na maendeleo ya wananchi.”
Akionyeshwa kutoridhishwa na kiwango cha uongozi cha baadhi ya madiwani mkoani humo, Rais Kikwete amewaambia viongozi hao: “Kazi ya madiwani haiwezi kuwa kupima na kugawa viwanja. Mliomba kazi ya udiwani ili kuwatumia wananchi na kuwaletea maendeleo. Nyie madiwani hamuwezi kuendelea kuwasibiri TASAF kuwaletea wananchi wenu maendeleo. Hii ni kazi yenu.”
Ameongeza kuelekeza Rais Kikwete: “Kazi yenu haiwezi kuwa ni kusubiri posho ya vikao na kupokea mishahara bure. Lazima muwe na tamaa ya maendeleo ya wananchi wenu.”
Aidha, aliwakumbusha kuwa Serikali inatoa fedha nyingi kwa halmashauri kwa ajili ya ujenzi wa barabara kwenye halmashauri hizo, lakini madiwani wanashindwa ama kuchelewa kuzitumia fedha hizo kujenga barabara hadi mwaka wa fedha unamalizika.
“Hili nalo halikubaliki. Kwa sababu Serikali inawapa fedha nyingi, lakini nyie hamzitumii kwa wakati na fedha hizo zinarudishwa kwenye Mfuko wa Barabara.”

No comments:

Post a Comment