Monday, September 23, 2013

ICC yamruhusu William Ruto kurejea Kenya



Ruto alifikishwa ICC kwa tuhuma za uhalifu dhidi ya binadamu
Majaji katika mahakama ya kimataifa kuhusu uhalifu wa kivita ICC wameahirisha kesi ya naibu Rais wa kenya William Ruto kwa juma moja ili kumpa mda kurejea nyumbani kushughulikia hali ya kiusalama inayokumba taifa hilo.
Watu wanoaminika kuwa magaidi wa Al Shabaab wameteka jumba la kifahari lenya maduka la Westgate jijini Nairobi na kuwazuilia mateka wakenya kadhaa.
Bwana Ruto anakabiliwa na mashtaka ya uhalifu wa kibinadamu kufuatia ghasia za baada ya uchaguzi wa 2007 nchini kenya.
Ruto na Rais Uhuru Kenyatta, wanakabiliwa na tuhuma za za uhalifu dhidi ya binadamu baada ya kudaiwa kuhusika na ghasia za kikabila baada ya uchaguzi wa mwaka 2007-2008 ambapo watu zaidi ya elfu moja waliuawa.
Mahakama iliakhirisha kesi baada ya kikao cha dharura kuitishwa huku upande wa mashtaka ukisema kuwa hauna pingamizi lolote ikiwa kesi zitaakhirishwa kwa muda mfupi.
Mwakilishi mmoja wa mashahidi aliangua kilio mahakamani na kutaka mahakama iweze kumruhusu Ruto kurejea nyumbani kushughulikia swala hilo la dharura.
''Kutokana na hali ilivyo na maoni tuliyoyasikia , mahakama inamruhusu Ruto kurejea nyumbani kwa muda wa wiki moja,'' alisema jaji anayesimamia kesi hiyo, Chile Eboe-Osuji.
"Kwa sasa Ruto ataruhusiwa kusalia Kenya kwa wiki moja, ila ikiwa atatoa ombi lengine,'' alisema jaji Chile.
Kwa mujibu wa wakili wa Ruto,Karim Khan, alitarajiwa kuondoka Uholanzi saa tatu asubuhi, saa za Afrika Mashariki

No comments:

Post a Comment