Wednesday, March 27, 2013

MASSAWE AWALILIA WANANCHI WA KAGERA

SERIKALI imeombwa kufanya utaratibu wa kuwalipa fidia baadhi ya wananchi wa manispaa ya Bukoba iliyoko  mkoani Kagera walioondolewa kwenye makazi yao  ili  kupisha upanuzi wa uwanja wa ndege uliko mjini  Bukoba.

Ombi hilo limetolewa na mkuu wa mkoa wa Kagera, Kanali mstaafu Fabian Massawe kwenye taarifa yake aliyoitoa kwa waziri wa uchukuzi Dr.Harrison Mwakyembe aliyekuwa mjini Bukoba kukagua maendeleo ya shughuli za upanuzi wa uwanja huo wa ndege.

Massawe amesema hadi sasa  ni wananchi 12 tu ambao wamelipwa fidia kwa ajili ya  kupisha upanuzi wa uwanja kati ya  41 waliofanyiwa tathimini, amesema wananchi hao mara kwa mara wamekuwa wakiandamana kudai haki yao kwenye ofisi yake.

Naye, mhandisi mshauri wa kampuni ya SSI inayosimamia ujenzi wa uwanja huo, Patrick Kain amemweleza waziri Mwakyembe sababu   zinazochangia kuchelewesha upanuzi wa uwanja huo wa ndege, ametaja sababu hizo kuwa ni pamoja na mvua zinazonyesha mara kwa mara katika mji huo na  ndege zinazoruka na kutua katika uwanja huo kutokuwa na ratiba maalumu.

Akizungumza baada ya kufanya ukaguzi wa  maendeleo ya shughuli za upanuzi wa uwanja, waziri wa uchukuzi  Dr.Harrison Mwakyembe amesema kuwa ameridhishwa na shughuli zinazofanywa za upanuzi wa uwanja huo , amesema serikali itaweka utaratibu wa kuondoa vikwazo anavyokutana navyo mkandarasi vinavyopunguza  kasi yake  ya upanuzi wa uwanja huo ili uweze kumalizika kwa wakati.

Ujenzi wa uwanja wa ndege wa Bukoba unatarajia kugharimu zaidi ya shilingi bilioni 21 na unatarajia kumalizika mwezi agosti, mwaka huu, katika ziara hiyo Waziri Mwakyembe aliambata na naibu waziri wake Dr. Charles Tizeba.

No comments:

Post a Comment