Wednesday, November 21, 2012

IHUNGO KWAWAKA MOTO MWALIMU WA KEMIA APINGWA

 Baadhi ya wanafunzi wakiandamana.
 Wanafunzi wa kidato cha sita na cha tano wakiwa nje ya jengo la manispaa ya Bukoba.
 Mkuu wa wilaya ya Bukoba Bi Ziporah Lion Pangani akiongea na wanafunzi shule ya sekondari ya Ihungo waliofanya maandamano.
 Wanafunzi wakisikiliza kwa makini.
WANAFUNZI wa kidato cha tano na sita wa shule ya sekondari Ihungo ambayo ni miongoni mwa shule kongwe hapa nchini iliyoko katika manispaa ya Bukoba wameandamana hadi kwenye ofisi ya mkuu wa wilaya ya Bukoba kupinga vitendo wanavyofanyiwa na baadhi ya walimu wao.

Wanafunzi hao waliandamana jana  hadi kwenye ofisi ya mkuu wa wilaya ya Bukoba Ziporah Pangani na kutoa malalamiko mbele yake kwa kile walichodai kuwa wanafanyiwa hujuma na mwalimu anayewafundisha somo la kemia waliyemtaja kwa jina la Philemon Tumwesige.


Kwa nyakati tofauti bila kutaja majina yao wakimlalamikia mwalimu Tumwesige walisema kuwa amekuwa ha tabia ya kutoingia darasani kuwafundisha somo hilo la kemia, walisema kuwa tangu mwaka huu wa sasa wa masomo uanze ameingia darasani mara 13  wakati katika kipindi hicho alitakiwa kuwa ameingia darasani mara 56.


Waliendelea kumlalamikia kwa kumueleza mkuu wa wilaya kuwa amekuwa na tabia ya kuwachangisha fedha ili aweze kuwafundisha, walisema mwalimu Tumwesige alikuwa akimtaka kila mwanafunzi amchangie shilingi 5,000 ili aweze kuingia darasani.


Walisema idadi kubwa wanafunzi walimchangia kiasi hicho, walimweleza mkuu huyo wa wilaya kuwa pamoja na kumchangia kiasi hicho cha fedha amekuwa akigoma kuwafundisha na mara kwa mara alikuwa akisema kuwa anafanya hivyo ili wanafunzi wa shule hiyo wasifaulu somo la kemia.


Wanafunzi hao walisema kinachodhihirisha mkakati wake wa kutaka wanafunzi wasifaulu mtihani wao wa kemia ni matokea ya mtihani wa majaribio wa somo la kemia uliofanywa na wanafunzi wa kidato cha sita katika shule hiyo, walisema kati ya wanafunzi zaidi ya 400 wa kidato cha sita waliofanya somo hilo la  kemia waliofaulu ni 17 tu.


Walimuomba mkuu wa wilaya afanye utaratibu ili wapatiwe mwalimu mwingine wa kemia, walisema kamwe mwalimu huyo awezi kuwapa elimu sahihi kwa kuwa wameishavutana naye sana, walisema kila siku wamekuwa wakimtolea taarifa kwa uongozi wa juu wa shule hiyo lakini hatua zimekuwa hazichukuliwi dhidi yake.


Mkuu wa wilaya Bi. Pangani aliwaahidi kushughulikia suala hilo haraka iwezekanavyo ili lipatiwe ufumbuzi, aliwaambia warudi shuleni watulie ili ofisi ya elimu iweze kushughulikia suala hilo, "Nendeni shuleni mtulie najua mnadai haki yetu na haki yenu itapatikana. Alimaliza.

No comments:

Post a Comment