Monday, February 25, 2013

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI TOKA IKULU


THE UNITED REPUBLIC OF TANZANIA
DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS


.
 
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete  leo Februari 24, 2013 ameungana na Wakuu wenzake wa Nchi za  Ukanda wa Maziwa Makuu  kutia  saini Mpango wa Umoja wa Mataifa wa Amani, Usalama na Ushirikiano katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) mjini Addis Ababa, Ethiopia.
Mhe. Rais Kikwete alisema mara baada ya utiwaji saini wa Mpango huo kwamba: “Hii ni siku kubwa na ya kihistoria kwa watu wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, jirani zake na Ukanda wote wa Maziwa Makuu. Ni siku ya kukumbukwa kwa Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC), Afrika, Umoja wa Afrika, Umoja wa Mataifa na Jumuiya yote ya Kimataifa.
“Watu wa Kongo wameteseka kwa muda mrefu sana. Wanastahili kupumua sasa. Wanastahili kuishi maisha bora; maisha ambayo usalama wao umehakikishiwa na kuthibitishwa; maisha ambayo yatawafanya waendeshe maisha yao kwa kufanya mambo ya maana zaidi katika kuboresha  maisha yao ya kila siku.
“Saini tulizotia kwa Mpango huo leo ni kielelezo cha  dhati na ahadi ya utekelezwaji wa  yale yanayotarajiwa na watu wa Kongo na Ukanda wa Maziwa Makuu kwa ajili ya Amani, Usalama na Ushirikiano.
“Kwa niaba ya Serikali na Watu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania naahidi kwamba sisi tutatekeleza kwa dhati yale yote yanayotarajiwa kwa upande wetu”, alisema.
Mpango huo umetiwa saini na viongozi kutoka   Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Jamhuri ya Uganda, Jamhuri ya Afrika ya Kati, Jamhuri ya Angola, Jamhuri ya Burundi, Jamhuri ya Kongo (Brazaville), Jamhuri ya Zambia, Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Jamhuri ya Afrika Kusini.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Mhe. Ban Ki-moon, Mwenyekiti wa Kamisheni ya Umoja wa Mataifa, Dkt. Nkosazana Dlamini-Zuma, pamoja na wenyeviti wa Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC) na Ukanda wa Maziwa Makuu (ICGLR) wametia  saini Mpango huo kama mashahidi na wadhamini.
Mpango huo una nia ya kuchangia juhudi ambazo zimefanywa na ICGLR na SADC katika kutafuta amani Mashariki ya Kongo na ukanda wote wa Maziwa Makuu kwa ujumla.
Mpango huo pia umetilia maanani mapendekezo muhimu yaliyokubalika baada ya mashauriano kati ya wakuu wa nchi za ICGLR  na SADCna Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa.
Mapendekezo ya mpango huo ni pamoja na kuboresha sekta ya Ulinzi na usalama, hususan jeshi la polisi, Kuimarisha mamlaka ya nchi hasa mashariki ya Kongo; na kuendeleza ajenda kuhusu maelewano, kuvumiliana na kudumisha demokrasia nchini humo.
Vile vile, nchi za Kanda zimetakiwa kutoingilia mambo ya ndani ya nchi jirani, kututoa msaada wowote wa vikundi vya waasi, kuheshimu utawala na maeneo ya nchi jirani na kuimarisha mahusiano ya Kanda.
Hali kadhalika, Jumuiya ya Kimataifa imetakiwa kuisaidia DRC na Kanda yote ya Maziwa Makuu kwa ujumla katika utekelezaji wa miradi muhimu pamoja na mkataba wa Amani, Usalama na Maendeleo katika Ukanda wa Maziwa Makuu.
Aidha, Mpango huo unapendekeza kuwepo kwa chombo cha usimamizi (Oversight Mechanism) ambacho kitaundwa na viongozi wote wa nchi 11 pamoja na Umoja wa Mataifa, SADC na ICGLR.

Imetolewa na:
Muhidin Issa Michuzi,
Mwandishi wa Habari wa Rais, Msaidizi,
Addis Ababa,
ETHIOPIA.
24 Februari, 2013

No comments:

Post a Comment