Wednesday, August 05, 2015

RAIS KIKWETE AWAAPISHA MAJAJI 14



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete leo, Jumatano, Agosti 5, 2015, amewaapisha Majaji 14 akiwamo Jaji mmoja wa Mahakama ya Rufani Tanzania katika sherehe iliyofanyika Ikulu, Dar es Salaam.

Rais Kikwete aliwateua majaji hao hivi karibuni katika mwendelezo wake wa kuhakikisha kuwa Muhimili wa Mahakama unakuwa na raslimali watu ya kutosha ili kuendelea kutoa haki kwa haraka zaidi na kwa ufanisi zaidi.

Walioapishwa leo katika sherehe iliyohudhuriwa pia na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mheshimiwa Mohamed Chande Othman ni pamoja na Jaji Richard Mziray ambaye anakuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania.

Majaji wengine ambao wote ni Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania ni Mheshimiwa Ignas Pius Kitusi, Mheshimiwa Lameck Michael Mlacha, Mheshimiwa Wilfred Peter Dyansobera,             Mheshimiwa Salima Mussa Chikoyo, Mheshimiwa Issa Kweka Arufani, Mheshimiwa Sirilius Betran Matupa na Mheshimiwa Julius Benedicto Malaba.

Wengine ni Mheshimiwa Victoria Lyimo Makani, Mheshimiwa Lucia Gamuya Kairo, Mheshimiwa Rehema Joseph Kirefu, Mheshimiwa Benhaji Shaaban Masoud, Mheshimiwa Issa John Maige na Mheshimiwa Adam Juma Mwambi.
Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu,
DAR ES SALAAM.

No comments:

Post a Comment