Sunday, November 29, 2015

WATUMISHI WENGINE WATATU WASIMAMISHWA KAZI TRA *Ni kupisha uchunguzi wa tuhuma zinazowakabili


SERIKALI imewasimamisha kazi watumishi watatu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ambao jana iliamriwa kwamba watahamishiwa mikoani. Watumishi hao ni Bw. Anangisye Mtafya, Bw. Nsajigwa Mwandengele na Bw. Robert Nyoni.

Uamuzi huo umetolewa leo (Jumamosi, Novemba 28, 2015), na Waziri Mkuu Majaliwa Kassim Majaliwa ili kupisha uchunguzi zaidi wa tuhuma zinazowakabili. Kama ilivyo kwa wenzao sita waliosimamishwa kazi jana (akiwemo aliyekuwa Kamishna Mkuu), nao pia hawaruhusiwi kusafiri kwenda nje ya nchi hadi uchunguzi utakapokamilika.

 “Kazi ya kuwachunguza ilianza jana ileile na sasa, tumeona hawa watu wanapaswa kuwa nje ya utumishi ili kupisha uchunguzi ufanyike kwa uhuru zaidi,” alisema Waziri Mkuu.

Pia Waziri Mkuu amemuagiza Kaimu Kamishna Mkuu wa TRA, Dkt. Philip Mpango atekeleze maagizo hayo kwa kuwaandikia barua watumishi hao.

Jana mchana, Waziri Mkuu alifanya ziara ya kushtukiza kwenye bandari ya Dar es Salaam akiwa na nia ya  kukagua namna shughuli zinavyoendelea kwenye bandari hiyo hasa kwenye maeneo ya kupokelea mizigo kutoka nje ya nchi.

Katika kikao kilichofanyika bandarini hapo na kuhudhuriwa na baadhi ya viongozi wa Serikali, Waziri Mkuu aliamua kuwasimamisha kazi maafisa watano na TRA kutokana na ‘upotevu’ wa makontena 349 yenye thamani ya zaidi ya sh. bilioni 80/-.

Waziri Mkuu alisema upotevu huo unasababishwa na mchezo unaofanyika baina ya wafanyabiashara na watumishi wa TRA ambao wanaruhusu makontena kupita bila kulipiwa ushuru na hivyo kuikosesha Serikali mapato.

(mwisho)

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
2 MTAA WA MAGOGONI,

No comments:

Post a Comment