Monday, March 02, 2015

HOTUBA YA MWISHO WA MWEZI FEBRUARI, 2015, YA MHESHIMIWA DKT. JAKAYA MRISHO KIKWETE, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, ILIYOTOLEWA TAREHE 1 MACHI, 2015






Ndugu Wananchi;
Kama ilivyo ada tunamshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kutuwezesha kuzungumza kupitia utaratibu wetu huu mzuri wa hotuba za kila mwisho wa mwezi.  Kwa mwisho wa mwezi wa Februari nina mambo matano ninayopenda kuyazungumzia. 
Zoezi la Uandikishaji Wapiga Kura
Ndugu Wananchi;
          Jambo la kwanza ni uandikishaji wa Wapiga Kura.  Tarehe 24 Februari, 2015 Waziri Mkuu, Mheshimiwa Mizengo Kayanza Peter Pinda alizindua rasmi uandikishaji wa wapiga kura ikiwa ni sehemu ya zoezi la uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura nchini.  Zoezi hili lilizinduliwa Makambako, Mkoani Njombe na litaendelea nchini kote mpaka litakapokamilika kwa mujibu wa ratiba itakayopangwa na Tume ya Uchaguzi.  Uandikishaji unatumia teknolojia ya kisasa ya utambuzi wa alama za vidole (BVR) na macho ya mtu anayeandikishwa.  Teknolojia hii itatusaidia kuondoa kutoaminiana, manung’uniko na madai kuhusu udanganyifu katika chaguzi zetu kwamba wamepiga kura wasiostahili.  Kuanza kutumika kwa teknolojia hii ni kielelezo cha utashi wa Serikali kuwa nchi yetu iwe na chaguzi zilizo huru, wazi na haki.
Ndugu Wananchi;
          Mtakumbuka kuwa, kabla ya uzinduzi wa zoezi hili, Tume ya Taifa ya Uchaguzi ilifanya zoezi la majaribio ya uandikishaji wa wapiga kura kwa kutumia mashine za teknolojia hii mpya katika kata 10 katika Halmashauri za Kinondoni, Kilombero na Mlele kati ya tarehe 15 hadi 23 Desemba, 2014. 
          Habari njema ni kuwa, kwa kutumia mashine za BVR, idadi ya waliojiandikisha ilivuka lengo la uandikishaji kwa kipindi kilichopangwa katika Kata hizo.  Katika Halmashauri ya Kilombero walioandikishwa walifikia asilimia 110.9 ya lengo, katika Halmashauri ya Mlele uandikishaji ulifikia asilimia 101 ya lengo na katika Jimbo la Kawe, katika Halmashauri ya Wilaya ya Kinondoni walioandikishwa walikuwa asilimia 105.67 ya lengo.    Mafanikio haya ni ya kutia moyo pamoja na changamoto za kiufundi zilizojitokeza na zile zinazotokana na upya wa mfumo wenyewe kwa watumiaji.  Changamoto hizo zimefanyiwa kazi na watengenezaji wa vifaa vinavyotumika katika awamu hii ya uandikishaji wa wapiga kura nchi nzima.
Ndugu Wananchi;      
Nimefarijika na taarifa kuwa zoezi la uboreshaji wa Daftari na uandikishaji wa wapiga kura limeanza vizuri Makambako.  Wananchi wamejitokeza kwa wingi kuliko ilivyotarajiwa.  Kati ya tarehe 23 hadi 25 Februari, 2015 kwa mfano, Tume ilitegemea kuandikisha wapiga kura 9,541 lakini kutokana na mwamko wa wananchi kuwa mkubwa wameweza kuandikisha wapiga kura 13,042.  Kila kituo kilikuwa kinaandikisha kati ya wapiga kura 80 na 150 kwa siku.  Lengo la Tume ni kuandikisha wapiga kura 32,000 katika Halmashauri ya Makambako ambako kwa siku wanatarajia kuandikisha watu 4,320.  Naambiwa kuwa hesabu za juzi na jana wameandikisha hadi wapiga kura 6,000 kwa siku.  Kwa kasi hii na kama mambo yatakwenda kama inavyotarajiwa, lengo hilo litafikiwa na hata kuvukwa.
Ndugu Wananchi;
          Hatuna budi kutoa pongeza kwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi kwa hatua hii ya kutia moyo tuliyofikia katika mchakato huu.  Inaondoa hofu iliyoanza kuingia miongoni mwa baadhi ya watu kuwa huenda zoezi hili lisingefanikiwa.  Tunachokitaka kwa Tume ni kuona zoezi hili linaendelea na kukamilika kama ilivyopangwa. Napenda kurudia ahadi niliyokwishaitoa kwa Tume kwamba Serikali itafanya kila linalowezekana kuiwezesha kirasilimali ili iweze kutimiza jukumu lake hilo.  Nimekwishawakumbusha Hazina kuhusu umuhimu wa zoezi hili kufanikiwa kama ilivyopangwa.  Hivyo basi, nimewataka wahakikishe kutoa kipaumbele cha kwanza katika mgao wa fedha.   Kama haifanyiki nawaomba Tume waniambie mimi mwenyewe.
          Wito wangu kwenu, wananchi wenzangu, ni kujitokeza bila ya kukosa kwenda kujiandikisha kwa mujibu wa ratiba ya uandikishaji katika maeneo yenu kama itakavyotolewa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi.  Msifanye ajizi maana hakutakuwepo na fursa nyingine ya kujiandikisha kabla ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu baada ya fursa hii kupita. 
Ndugu Wananchi;
Kama ilivyoelezwa na Tume na mimi kusisitiza mara kadhaa kuwa watakaojiandikisha wakati huu ndio watakaopiga kura ya maoni kuhusu Katiba Inayopendekezwa na ndio watakaopiga kura katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, mwaka huu.  Vitambulisho vya zamani vya mpiga kura havitatumika, hivyo watu wote ambao ni Watanzania na wana umri wa miaka 18 au zaidi lazima wajitokeze kuandikishwa upya. Watu pekee ambao hawatapaswa kujiandikisha tena ni wale tu walioandikishwa katika zoezi la majaribio lililofanyika katika zile kata 10 za Halmashauri za Kinondoni, Ifakara na Mlele mwezi Desemba, 2014.  Vitambulisho walivyopata ndivyo vyenyewe.
Ndugu Wananchi;
          Napenda kutumia nafasi hii pia kuwaomba viongozi wa vyama vya siasa, Serikali, dini na asasi za kiraia kuungana na Serikali na Tume ya Uchaguzi katika kuwakumbusha na kuwahamasisha wananchi wakajiandikishe.  Naomba tusiwachanganye wananchi kwa kutoa taarifa zisizokuwa za kweli na kuwafanya wakaacha kujiandikisha. Sisi katika Serikali tunafanya kila linalowezekana kuhakikisha kuwa kila atakayejitokeza kujiandikisha anaandikishwa. Aidha, tutahakikisha kuwa kila panapojitokeza changamoto zinatafutiwa ufumbuzi kwa wakati mwafaka. 
Tunatambua kuwa mfumo huu ni mpya hivyo panaweza kujitokeza changamoto zinazosababishwa na upya wake.  Nawaomba wahusika kuendelea kuwaelimisha watendaji wanaohusika ili wapate uzoefu unaostahili.  Aidha, nawasihi wananchi kuwa wavumilivu na waelewa pale ambapo wakati mwingine watalazimika kukaa kwenye mistari kwa muda mrefu kusubiri kujiandikisha, au wakalazimika kuja siku ya pili.
Ndugu Wananchi;
 Kupiga kura kuamua kuhusu Katiba Inayopendekezwa au kuchagua Rais, Wabunge na Madiwani ni haki na wajibu wa kila raia.  Lakini, kuipata haki hiyo na kuweza kutimiza wajibu huo kunategemea kuwa na kitambulisho cha mpiga kura.  Bila ya hivyo haiwezekani.  Haya shime jitokezeni, mjiandikishe, ili muweze kuitumia haki yenu na kutimiza wajibu wenu wa kuipigia kura Katiba Inayopendekezwa na kuchagua viongozi mnaowaona wanafaa kuongoza nchi yetu, jimbo lako na kata yako.
Kura ya Maoni
Ndugu Wananchi;
          Jambo la pili ninalotaka kulizungumzia ni kuhusu Kura ya Maoni ya Katiba Inayopendekezwa.  Kama mjuavyo, baada ya Bunge Maalumu la Katiba kutunga Katiba Inayopendekezwa na Rais kuchapisha Katiba hiyo katika Gazeti la Serikali na kutangaza siku ya kupiga kura ya maoni, kinachoendelea sasa ni matayarisho ya kufanyika kwa kura hiyo.  Yapo majukumu ya Serikali, yapo majukumu ya Tume ya Uchaguzi, na yapo majukumu ya Serikali na Tume kwa pamoja.  Utekelezaji umeishaanza na unaendelea.  Miongoni mwa mambo yanayotakiwa kufanyika ni uandikishaji wa wapiga kura ambao umekwishaanza na unaendelea.
 Ipo pia kazi ya kuchapisha na kusambaza Katiba Inayopendekezwa ili wananchi waweze kuisoma na kuielewa kabla ya kupiga kura ya maoni.  Tayari Katiba Inayopendekezwa imetangazwa katika tovuti za Wizara ya Katiba na Sheria, Wizara ya Habari, Utamaduni, Vijana na Michezo na katika tovuti ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali.  Pia imechapichwa magazetini. 
Hadi tarehe 27 Februari, 2015 vitabu 1,558,805 vilikuwa vimechapishwa na nakala 1,341,300 kusambazwa.  Nakala 1,141,300 zimesambazwa kwenye mikoa 25 ya Tanzania Bara na nakala 200,000 zimegawiwa kwa Zanzibar.  Kwa upande wa Tanzania Bara kila Kata imepewa vitabu 300.  Kwa vile Kata zina wastani wa vijiji vitano (5) hii ina maana kwamba kila kijiji kimepata vitabu 60 kwa kila kijiji ambayo si haba. 
Ndugu Wananchi;
Tume ya Uchaguzi itatoa maelekezo kuhusu utaratibu wa kutoa elimu kwa umma.  Nimeambiwa tayari asasi za kiraia 420 kwa upande wa Bara na 75 kwa upande wa Zanzibar zimejiandikisha kwa ajili ya zoezi hilo. Halikadhalika, Tume itatoa maelekezo husika kuhusu kampeni ya Kura ya Maoni wakati ukiwadia.  Naomba watu wawe na subira na kuzingatia masharti ya Sheria ya Kura ya Maoni na Kanuni zake.  Tukifanya hivyo, zoezi hili muhimu na la kihistoria litatekelezwa kwa usalama na utulivu.  Watu watafanya uamuzi kwa uhuru, uelewa, amani na usalama.  
Hali ya Usalama Nchini
Ndugu wananchi;
          Jambo la tatu ninalotaka kulizungumzia ni hali ya usalama nchini.  Kwa jumla hali ya usalama ni nzuri, hata hivyo kuna matukio ya kiusalama ambayo ningependa kuyazungumzia.  La kwanza ni mashambulizi yenye sifa za ujambazi na mwelekeo wa kigaidi.  Na, la pili ni la mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi.
Katika kipindi cha miezi 12 hivi kumekuwa na matukio ya watu kuvamia vituo vya Polisi, wengine wanachoma moto au wengine wanapora silaha.  Pia kumekuwepo na matukio ya kuwashambulia Polisi walioko kwenye doria na wengine kuporwa silaha.  Vituo vya Polisi vilivyovamiwa na silaha kuporwa ni vya Newala Mkoani Mtwara silaha tatu ziliporwa, Ikwiriri katika Wilaya ya Rufiji silaha saba, Kimanzichana, Wilaya ya Mkuranga silaha tano, mbili za polisi na tatu za raia waliokwenda kuzihifadhi pale, na Ushirombo Wilaya ya Bukombe silaha 18.  Pugu Machinjioni na Tanga, askari waliokuwa katika shughuli za ulinzi na doria walishambuliwa na kuporwa silaha tatu.  Kule Songea kulikuwepo na matukio mawili ya Polisi kushambuliwa lakini silaha hazikuporwa.
Bahati mbaya, vijana wetu saba wa Jeshi la Polisi walipoteza maisha katika matukio hayo.  Newala alikufa Polisi mmoja, Kimanzichana mmoja, Ikwiriri wawili, na Ushirombo watatu. Wapo Polisi kadhaa waliopata majeraha ya namna mbalimbali katika mashambulizi haya. 
Ndugu Wananchi;
Silaha zote 18 zilizoporwa Ushirombo zimepatikana na watu 10 wanaotuhumiwa kuhusika na uhalifu huo wamekamatwa.  Katika tukio la Tanga silaha moja kati ya mbili zilizoporwa imepatikana.  Watuhumiwa saba wametiwa mbaroni, wanne  kati yao ni wale waliokuwa wamejifisha katika mapango ya Kiomoni katika Kitongoji cha Karasha-mikocheni, kilichoko kijiji cha Mzizima wilayani Tanga. Tayari watu wanne wanaotuhumiwa kuhusika na tukio la Ikwiriri wamekamatwa.  Polisi wanaendelea na upelelezi kuwapata watu wengine na kuzipata silaha saba zilizoporwa kituoni hapo.  Kwa tukio la Newala silaha zote tatu zimepatikana pamoja na bastola moja ya mtuhumiwa aliyehusikaa  na watu wawili wametiwa nguvuni.  Hali kadhalika, upelelezi unaendelea wa kuzipata silaha zilizoporwa ambazo hazijapatikana mpaka sasa: yaani Kimanzichana moja, Pugu Machinjioni moja na Tanga iliyosalia moja. 
Ndugu Wananchi;
          Matukio haya yana sura mbili.  Yana sura ya ujambazi, lakini pia baadhi yake yana dalili za ugaidi.  Vyombo vyetu vya usalama vinaendelea kufanya kazi yake ya uchambuzi wa kila tukio na kulipa nafasi yake stahiki.  Napenda kutumia nafasi hii kutoa pongezi za dhati kwa Jeshi la Polisi wakishirikiana na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania na vyombo vingine vya usalama kwa kazi kubwa na nzuri waifanyayo kupambana na uhalifu nchini.  Mafanikio tunayaona, kama nilivyoeleza na kama tulivyosikia kule Tanga hivi karibuni ni matunda ya ushirikiano huo.  Hata hivyo, nimewataka waendelee kuwasaka watu hawa waovu po pote walipo ili wafikishwe mahakamani na kuzirejesha mikononi mwa Polisi silaha zote zilizoporwa. 
Nawaomba wananchi wenzangu wote kushirikiana kwa karibu na vyombo vya usalama hususan Jeshi la Polisi ili tuweze kupata mafanikio zaidi dhidi ya uhalifu huu na uhalifu mwingineo. Nawaomba mfanye mambo mawili:  Kwanza, toeni taarifa Polisi mnapozipata habari za vitendo viovu au nyendo za watu waovu wanavyokusudia kufanya wahalifu au taarifa za wale waliokwishafanya uhalifu. 
Pili, naomba watu waache kuwashabikia watu hawa waovu wala kueneza taarifa zao potofu kwenye mitandao ya kijamii.  Badala yake tutumie mitandao ya kijamii kuponda fikra zao potofu, fikra zao hasi na vitendo vyao viovu pamoja na kuwafichua wao na mambo yao mabaya wayafanyo.  Napenda kutumia nafasi hii kuwashukuru na kuwapongeza wananchi wote walioweza kutoa taarifa zilizowezesha kuzuia uhalifu usifanyike au zilizowezesha kutiwa mbaroni kwa wahutumiwa wa vitendo vya ujambazi na ugaidi.    Hatuwezi kushinda uhalifu bila ushirikiano baina ya wananchi na vyombo vya ulinzi na usalama.

Mauaji ya Watu Wenye Ulemavu wa Ngozi
Ndugu wananchi;
          Nimesikitishwa sana na taarifa kuwa mauaji ya ndugu zetu wenye ulemavu wa ngozi (Albino) yameibuka upya baada ya hali kuwa tulivu mwaka 2011.  Mwaka jana (2014) yalitokea matukio matatu katika mikoa ya Mwanza, Tabora na Simiyu na mwaka huu limetokea tukio moja mkoani Geita.
Lazima tulaani vikali mauaji ya ndugu zetu albino.  Ni vitendo vya kinyama ambavyo havitegemewi kufanywa au kutokea katika jamii yeyote ya watu waliostaarabika, ya watu wanaomuabudu Mungu.  Watu wenye ulemavu wa ngozi ni wanadamu wenzetu, wenye haki sawa ya kuishi na kupata hifadhi ya maisha yao kama walivyo wanadamu wengine.  Hawastahili kufanyiwa wanayofanyiwa.  Hawapaswi kuishi kwa hofu katika kijiji chao, mtaa wao au katika nchi yao.  Jamii nzima na sisi sote mmoja mmoja na katika umoja wetu, tunao wajibu wa kuhakikisha usalama wa maisha yao na mali zao kama ilivyo  kwa watu wengine wote. 
Kwa kweli, mauaji ya albino ni jambo linalofedhehesha na kulidhalilisha taifa letu.  Ni vitendo visivyovumilika.   Hatuna budi sote kushikamana na kuhakikisha kuwa tunapambana nao kisawasawa na kuwashinda.  Tusikubali kamwe wakaturudisha kule kubaya tulikokuwa zamani.    Naungana na Chama cha Albino Tanzania kulaani ukatili huu na kutaka watu wote wanaojihusisha na ukatili huu wasakwe, wakamatwe, wafikishwe Mahakamani na kupewa adhabu kali inayowastahili wanapopatikana na hatia. 
Ndugu Wananchi;
Napenda kuwahakikishia kuwa wakati wote Serikali imelipa uzito mkubwa suala la kudhibiti na kukomesha mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi au kukatwa baadhi ya viungo vyao wenyewe wakiwa hai.  Tumefanya hivyo bila ya kuchoka tangu tukio la kwanza baada ya mimi kuingia madarakani Aprili 17, 2006 na miezi mitatu tu  kule Nyahunge, Geita alipouawa Alfa Amon ambapo watuhumiwa wawili waliuawa na raia.  Mwaka 2007 kulikuwa na matukio saba.  Mwaka 2008 ndio ulikuwa mwaka mbaya sana walipouawa watu 18. 
Kutokana na jitihada kubwa zilizofanywa na Serikali kwa kushirikiana na wananchi mauaji yalipungua na kuwa tisa mwaka 2009.  Mwaka 2010 kukawa na tukio moja na mwaka 2011 hapakuwepo na tukio lolote.  Mwaka 2012 kukawa na tukio moja, mwaka 2013 aliuawa mtu mmoja na wawili kujeruhiwa.  Mwaka 2014 waliuawa watu watatu na wawili kujeruhiwa, na Januari, 2015 kumetokea tukio moja kule Geita. 
Ndugu Wananchi;
          Tangu mwaka 2006 mpaka 2015, watuhumiwa 139 wametiwa nguvuni, miongoni mwao wako watuhumiwa 16 wa matukio ya Desemba na Januari mwaka huu. Mashauri 35 yamefunguliwa mahakamani na kati ya hayo 10 bado yanaendelea na yapo katika hatua mbalimbali.  Watuhumiwa 73 wameachiliwa na 15 wamepatikana na hatia.  Kati ya hao waliopatikana na hatia 13 wamehukumiwa kifo na wawili wamepata kifungo cha miezi 6.  Watuhumiwa kwa matukio sita bado wanasakwa.
          Matukio ya mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi yametokea katika mikoa kumi kati ya mikoa 30 hapa nchini.  Mikoa hiyo ni hii ifuatayo:  Mwanza matukio 13, Kagera sita, Tabora matano, Geita manne, Mara manne, Kigoma manne, Simiyu matatu, Shinyanga mawili, Arusha moja na Mbeya moja.  Utaona matukio 41 kati ya 43 yametokea katika ukanda wa ziwa ambapo pia wanaongoza kwa mauaji ya vikongwe na wanawake kwa sababu za ushirikina. 
Ndugu Wananchi;
          Inawezekana kuwa matukio ya hivi karibuni yanaashiria kuwa uhalifu huu unataka kuibuka upya. Napenda kuwahakikishia ndugu zetu wenye ulemavu wa ngozi na Watanzania kwa jumla, kuwa hatutaacha hali iwe mbaya kama ilivyokuwa miaka ya nyuma.  Tutatumia mbinu na maarifa tuliyoyatumia kukabili wimbi kubwa la mauaji lililokuwepo mwaka 2007 na 2008 na kwa sababu hiyo tukaweza kupunguza hadi kufikia kutokuwa na tukio lolote la mauaji mwaka 2011. 
Tunachokiomba kutoka kwa wananchi ni ushirikiano na msaada wa kuwafichua watu wanaofanya vitendo vya mauaji na kukata viungo vya watu wenye ulemavu wa ngozi.  Pia wasaidie kutoa taarifa kuhusu wanunuzi wa viungo hivyo na waganga wanaochochea mahitaji ya viungo vya albino.  Ushirikiano wa wananchi wa wakati ule uliwezesha kupatikana kwa mafanikio niliyaeleza.  Naamini safari hii tukifanya hivyo tutafanikiwa pia.
Ndugu Wananchi;      
Kutokomeza kabisa matukio ya mauaji na ukataji wa viungo vya watu wenye ulemavu wa ngozi ni jambo linalowezekana.  Hata hivyo, litategemea watu kuacha imani za ushirikina.  Imani potofu, ati kuwa mtu akiwa na kiungo cha mtu mwenye ulemavu wa ngozi atafanikiwa katika shughuli zake za biashara, uvuvi na uchimbaji wa madini ndicho kichocheo cha uovu wote huu unaoendelea.  Ni ujinga ulioje kwa mtu kuamini kuwa mafanikio yake hayatategemea juhudi zake na maarifa yake bali kuwa na kiungo cha mwanadamu mwenzake mwenye ulemavu wa ngozi. 
Nilisema katika hotuba yangu ya mwisho wa mwezi Machi, 2008 kwamba, kama kuwa na kiungo cha albino ndiko kutakakomfanya mtu kufanikiwa katika shughuli zake za kibiashara na kiuchumi basi ndugu zetu wenye ulemavu wa ngozi wangekuwa ndiyo matajiri wakubwa nchini na duniani.  Maana wao sio tu wana viungo bali wana mwili mzima.    Kwa sababu ya kuwepo imani hizi za hovyo, juhudi za kuelimisha jamii kuachana na imani hizi potofu ziongezwe.  Naomba hili ndilo liwe jambo la msingi katika mapambano haya.  Tukifanikiwa katika hili, matatizo yote haya yatakoma.  Serikali na jamii haitalazimika kushughulikia mambo haya ambayo siyo tu ni fedheha hata kumsimulia mtu bali yanatisha na kusikitisha.
Ndugu Wananchi;
          Wiki ijayo nitakutana na baadhi ya viongozi na wanachama wa Chama cha Watu Wenye Ulemavu wa Ngozi.  Nimekubali maombi yao ya kukutana nao ili niweze kusikiliza maoni yao na tubadilishane mawazo juu ya namna bora ya kumaliza tatizo hili.  Mimi naamini kuwa ushirikiano wa karibu kati ya Serikali na jamii utatuwezesha kutokomeza mauaji ya ndugu zetu wenye ulemavu wa ngozi na kuliondolea taifa letu aibu hii.
Ziara ya Zambia
Ndugu Wananchi;
          Tarehe 25 na 26 Februari, 2015 nilifanya ziara ya siku mbili ya kiserikali nchini Zambia kwa mwaliko wa Rais mpya wa nchi hiyo, Mheshimiwa Edgar Lungu.  Ziara ilikuwa na mafanikio makubwa.  Mimi na ujumbe wangu tulifarijika sana kuona kuwa mawazo ya nchi zetu mbili yanashabihiana sana kuhusu namna ya kuimarisha na kuboresha uhusiano wetu na ushirikiano na uhusiano wa nchi zetu mbili.  Kimsingi tumekubaliana katika masuala yote muhimu tuliyoyazungumza.    
Kuhusu TAZARA tumekubaliana kuchukua hatua thabiti kutatua matatizo ya kiungozi, kifedha na kiufundi yanayolikabili shirika letu hilo hivi sasa.  Tumeelewana kuwa hatuna budi kufanya marekebisho ya kimfumo na kiutendaji ili kutatua matatizo ya kimuundo na kimenejimenti yanayochangia kuzorota kwa ufanisi wa Shirika.    Tumekubaliana pia kuwa, Serikali zetu mbili zitekeleze ipasavyo wajibu wake kwa TAZARA ikiwa ni pamoja na kutoa mchango wake wa fedha kwa ajili ya kulifufua Shirika hili muhimu kwa uchumi wa nchi zetu mbili.
Ndugu Wananchi;
Tumekubaliana pia, kwamba, tuangalie uwezekano wa kuruhusu makampuni au mashirika mengine ya reli kutumia reli ya TAZARA kusafirishia mizigo yao kwa kulipa ushuru kwa TAZARA kwa huduma hiyo.  Tumeagiza Baraza la Mawaziri kulifanyia kazi wazo hili jema ili litekelezwe mapema iwezekanavyo. 
Kwa upande wa sekta ya nishati, tumekubaliana  kuwa, nchi zetu mbili ziendelee kushirikiana kuimarisha bomba la mafuta la TAZAMA. Ndugu zetu wa Zambia walitueleza dhamira yao ya kutaka kujenga bomba la kusafirisha gesi kutoka Dar es Salaam hadi Zambia.  Wameomba tukubali kuwauzia gesi asilia.  Niliwaeleza ni jambo linaowezekana, tumekubaliana nchi zetu zilifanyie kazi ombi hilo.
Serikali ya Zambia, imeahidi kuimarisha njia ya umeme kutoka Kasama hadi Mbala Zambia inakoanzia njia inayoleta umeme Sumbawanga.  Kufanya hivyo kutaondoa matatizo ya sasa ambapo umeme unaofika Sumbawanga kutoka Mbala huwa mdogo kiasi kwamba hauna nguvu ya kutosha kwa matumizi ya nyumbani, maofisini na viwandani.  Kwa sababu hiyo, hata mpango wa kuupeleka umeme huo Namanyere, Nkasi na Mpanda haukuweza kutekelezwa kama ilivyokuwa imekusudiwa awali.
Ndugu Wananchi; 
Kuhusu kuboresha huduma kwa abiria na mizigo katika mpaka wa Tanzania na Zambia pale Tunduma, tumekubaliana kuwa, Serikali ya Tanzania ikamilishe ujenzi wa jengo  litakalowezesha huduma zote muhimu za mpakani kutolewa katika jengo hilo (One Stop Border Post).  Wakati tunasubiri kukamilisha ujenzi huo, tumekubaliana tuwe na jengo la muda la kurahisisha taratibu za usafiri wa abiria na usafirishaji wa mizigo katika mpaka wetu na Zambia.
Vilevile, tulizungumzia njia za kuimarisha na kuboresha taratibu za forodha kwa mizigo itokayo bandari ya Dar es Salaam kwenda Zambia na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo kupitia Zambia.  Tumekubaliana kuwa, Mamlaka ya Kodi ya Mapato ya Zambia iangalie uwezekano wa kuwaweka maafisa wake katika Bandari ya Dar es Salaam kama inavyofanyika kwa nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.  Hii itarahisisha taratibu za forodha kwa bidhaa za Zambia katika bandari yetu.  Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo imeshaanza mchakato wa kupata fursa hiyo.  Kwa jumla, ziara ilikuwa ni yenye mafanikio makubwa.
Rambirambi
Ndugu Wananchi;
          Wakati tulipokuwa tunajiandaa kurekodi hotuba hii tukapata habari ya huzuni na majonzi makubwa ya kifo cha Mbunge wa Mbinga Magharibi, Mheshimiwa Capt. John Damian Komba.  Kifo chake kimeliondolea taifa letu mmoja wa viongozi wake wazuri, msanii mahiri, raia mwema na mzalendo wa kweli.  Marehemu alitumia muda mwingi wa maisha yake kuelimisha jamii kuhusu mambo mema, amefanya hivyo akiwa mwalimu na baadaye Kiongozi wa Kikundi cha Sanaa cha JWTZ na hapa mwishoni kiongozi wa kikundi cha Tanzania One Theatre cha Chama Cha Mapinduzi.  Kwa kutumia kipaji alichojaaliwa na Mola wake ametoa mchango mkubwa kwa maendeleo ya nchi yetu na ustawi wa Chama Tawala.  Daima tutamkumbuka kwa mambo mengi mema aliyoifanyia jamii ya nchi yetu na taifa kwa jumla.
Ndugu Wananchi;
          Katika salamu zangu za rambirambi kwa Spika wa Bunge na Katibu Mkuu wa CCM niliwaomba kupitia kwao salamu ziwafikie Wabunge wote na viongozi na wanachama wa Chama Cha Mapinduzi.  Hali kadhalika, niliomba kupitia kwao salamu ziwafikie familia ya marehemu Capt. John Komba.  Kwa familia ya ndugu yetu mpendwa, napenda  kuwahakikishia kuwa tuko pamoja nao katika kipindi hiki kigumu cha majonzi na maombolezo.  Tunawaombea kwa Mola awape moyo wa subira na uvumilivu.  Wananchi wa Wilaya ya Nyasa tunawapa pole nyingi kwa msiba mkubwa uliowakuta na pengo kubwa mlilolipata.  Nawaomba watambue kuwa namna bora zaidi ya kumlilia Mbunge wao aliyewapenda ni kudumisha mema yote aliyofanya na kukamilisha zile kazi ambazo alikusudia kuzifanya lakini hakuweza kufanya hivyo kwa sababu ya kukutwa na umauti.
          Mwisho nawaomba, Watanzania wote tuungane na familia yake kumwombea marehemu Capt. John Damian Komba mapumziko mema.  Amin.

Mungu Ibariki Afrika!
Mungu Ibari ki Tanzania!

Asanteni kwa kunisikiliza.

SERIKALI KUMALIZA DENI LOTE LA MAHINDI MACHI 30


SERIKALI imesema itajitahidi kuhakikisha inalipa deni lote la mahindi yaliyonunuliwa kutoka kwa wakulima na Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) ifikapo Machi 30, mwaka huu.

Akizungumza na maelfu ya wananchi kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika jana (Jumapili, Machi 2, 2015) kwenye uwanja wa CCM wa Vwawa wilayani Mbozi, Waziri Mkuu Mizengo Pinda alisema Serikali imedhamiria kufuta deni lote.

“Hapa Mbozi tulikuwa tunadaiwa sh. bilioni 21 lakini tumetoa sh. bilioni 4.5 kwa hiyo tutabakia na deni la kama sh. bilioni 16 ambalo tunajitahidi liwe limeisha ifikapo mwishoni mwa mwezi huu,” alisema.

“Tunachoweza kuahidi kama Serikali ni kwamba, msimu huu hatutarudia kosa la mwaka jana ingawa mtihani mkubwa tulionao ni wa kushughulika na hifadhi ya chakula kwa kujenga vihenge (SILOS) ili hata kama kuna ziada n tusipate taabu ya kuhifadhi,” aliongeza.

Alisema alishakwenda Poland kwa maelekezo ya Rais Jakaya Kikwete na wao wameshakuja kuona hali halisi ilivyo. “Tumependekeza vihenge vijengwe kwenye kanda za Mbeya, Rukwa, Dodoma, Dar es Salaam, Arusha au Kilimanjaro na Shinyanga ili iweze kuhudumia kanda ya Ziwa,” alisema.

Wakati huo huo, Mbunge wa Mbozi ambaye pia ni Naibu Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Bw. Godfrey Zambi amesema Serikali imekwishalipa zaidi ya sh. bilioni 81 na kwamba deni lililosalia linafikia sh. bilioni 59.

“Hadi mwishoni mwa mwaka jana, tulikuwa tumeshalipa sh. bilioni 51.5/- na mwaka huu tumepata sh. bilioni 15 kutoka CRDB na hivi majuzi kuna bilioni nyingine 15 zimetoka Hazina… Agizo la Serikali ni kwamba mahindi yote yawe yamelipwa ifikapo Machi 30, naamini tutakamilisha,” alifafanua.

Alielezea pia tatizo la maji linaloukabili mji wa Mbozi na vitongoji vyake na kueleza kwamba Serikali inashughulikia tatizo hilo katika programu mbalimbali.

Mapema, akiwa katika ghala la nafaka la NFRA katika makao makuu ya wilaya ya Mbozi, Vwawa, Waziri Mkuu alielezwa kwamba kanda ya Makambako ambayo inajumuisha vituo vya Makambako na Vwawa imezidiwa uwezo na sasa wanalazimika kuhifadhi magunia ya mahindi nje kwa vile maghala yamejaa.

Meneja wa Kanda hiyo wa NFRA, Bw. Abdillah Nyangasa alisema kanda hiyo ina uwezo wa kuhifadhi tani za nafaka 34,000 ambapo kati ya hizo, tani 22,000 ni maghala ya Makambako na tani 12,000 ni maghala ya Vwawa, Mbozi.

Hata hivyo, Bw. Nyangasa alisema kanda hiyo kwa sasa kina tani za mahindi 79,496.8 zikijumuisha tani 15,738.9 za msimu uliopita licha ya tani 63,757.8 ambazo zimenunuliwa katika msimu huu.

“Ili kukabiliana na uhaba wa maghala, kanda yetu hulazimika kufanya hifadhi ya nje (outside storage) kwa kutumia maturubai (tarpaulins) ili mahindi yasiharibiwe na hali ya hewa kama mvua au jua kali,” alisema Bw. Nyangasa.

Waziri Mkuu anamaliza ziara yake ya siku saba mkoani Mbeya leo kwa kufanya majumuisho na kisha kurejea jijini Dar es Salaam.



IMETOLEWA NA
OFISI YA WAZIRI MKUU

WAZIRI MKUU AWAJULIA HALI MAJERUHI WA AJALI MBEYA



WAZIRI MKUU Mizengo Pinda amewatembelea askari wa Jeshi la Polisi waliolazwa kwenye Hospitali ya Mkoa wa Mbeya kutokana na ajali waliyoipata jana wakati msafara wake ukielekea Kata ya Galula wilayani Chunya.

Waziri Mkuu aliwatembelea majeruhi hao na kuwapa pole leo asubuhi (Jumapili, Machi Mosi, 2015) kabla ya kuelekea wilayani Mbozi kuendelea na ziara yake ya Mkoa wa Mbeya. Alifuatana na mkewe Mama Tunu Pinda, Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Bw. Abbas Kandoro na Mganga Mkuu wa Mkoa huo, Dk. Seif Mhina.

Akizungumzia hali ya majeruhi hao, Mganga Mfawidhi wa Hospitali hiyo, Dk. Ismail Macha alisema jana walipokea majeruhi tisa lakini watatu walifanyiwa uchunguzi wa afya zao na kuruhusiwa na wengine sita ilibidi wawalaze na kuwafanyia uchunguzi zaidi kutokana na hali zao zilivyokuwa.

“Wengi wao walipata zaidi mshtuko ndiyo maana tukaamua kuwalaza ili tuendelee kuwapa uangalizi wa karibu… Mmoja tu ndiye amevunjika mkono wa kulia lakini wengine walipata michubuko miguuni, mikononi na usoni,” alisema.

Aliwataja waliolazwa kuwa ni Deogratius Nandi (31), Paulin Masolwa (27), Omary Hussein (24), Hamisi Haji (29) ambao wote ni wanaume. Majeruhi wa kike ni Cecilia Mussa Kabona (28) na Mwazanije Hassan (23) ambaye amevunjika mkono wa kulia. Waliopata matibabu na kuruhusiwa ni Mashaka Shabani (42), Khalifa Rashid (26) na Joel Cheja (21).

Dk. Macha alisema wanatarajia kuwaruhusu leo mchana ama kesho asubuhi kwani hali zao zinaendelea vizuri.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Ahmed Msangi alisema chanzo cha ajali hiyo ni vumbi na kokoto barabarani ambazo zilifanya gari hilo la FFU lisesereke na kupinduka. Hata hivyo, alisema mwendo mdogo wa gari hilo ulisaidia kuokoa maisha ya askari hao.

“Ajali ilitokea saa 5:30 asubuhi eneo la Chang’ombe ya Mjele. Eneo lile lina kokoto kubwa kubwa ambazo zilisababisha gari lao kuserereka na kupinduka… gari halikuwa kwenye mwendo mkali ndiyo maana askari hao wamepata majeraha madogo madogo,” alisema.

Waziri Mkuu leo anaendelea na ziara yake mkoani Mbeya kwa kutembelea wilaya ya Mbozi ambapo mbali ya kuzungumza na wananchi, atazindua maabara Vwawa sekondari, atakagua ghala la nafaka la NFRA na kupokea taarifa ya uzalishaji na usambazaji wa miche ya kahawa kwenye kituo cha TACRI - Mbimba.



IMETOLEWA NA
OFISI YA WAZIRI MKUU
JUMAPILI, MACHI MOSI, 2015

UTORO, MIMBA: CHUNYA NI ZAIDI YA KYELA Watoto 4,220 waguswa, Waziri Mkuu akemea tabia hizo






WAZIRI MKUU Mizengo Pinda ameendelea kukemea tabia za utoro na mimba kwa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari wilayani Chunya baada ya kupewa taarifa kwamba watoto 4,420 walitoroka shule na wengine 201 kupata mimba.

Februari 26, mwaka huu, Waziri Mkuu aliwaagiza Mkuu wa Wilaya ya Kyela pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo kuwasaka na kuwakamata wale wote waliohusika na utoro na ujauzito wanafunzi na kuwafikisha mahakamani mara moja ili liwe fundisho kwa wengine baada ya kuelezwa kwamba wanafunzi 94 walipata ujauzito na wengine 645 kuacha shule kwa sababu ya utoro.

Akizungumza na maelfu ya wananchi kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika jana (Jumamosi, Februari 28, 2015) kwenye uwanja wa Saba Saba wilayani Chunya, Waziri Mkuu alisema haiwezekani kuiacha hali hiyo iendelee huku watoto wa wilaya hiyo wakiharibiwa maisha kwa kukosa masomo.

“Utoro kwenye shule za msingi, taarifa ya wilaya inaonyesha watoto 1,979 waliacha shule kati ya mwaka 2010 na 2014 ambao ni wastani wa watoto 395 kila mwaka na katika suala la mimba, taarifa hiyo inasema watoto 161 waliachishwa shule kwa sababu ya ujauzito,” alisema.

“Haiwezekani kabisa! Hivi akinababa kuamua kutembea na mtoto shule ya msingi ni lipi hasa unalolitaka kwake… unamwachisha shule mtoto kwa lipi hasa, hapana. Nimeshatoa agizo wahusika wakamatwe. Wa zamani tunaweza tusiwapate, lakini hawa wa mwaka jana kwa shule za msingi wako 28, RC na watendaji wako fuatilieni na muwapeleke kwenye vyombo vya sheria,” alisisitiza.

Akichanganua takwimu za sekondari, Waziri Mkuu alisema kati ya mwaka 2010 na 2014 wanafunzi 2,251 waliacha shule kwa sababu ya utoro na wengine 40 waliachishwa kwa sababu ya ujauzito.

“Ninawasishi wazazi  na uongozi wa wilaya na mkoa tufanye jitihada kuhakikisha jambo hili linakomeshwa mara moja. Huwezi kununua madaftari an kumlipia ada tu halafu usitake kuona mwanao anamaliza shule. Kila mzazi ana jukumu la kuhakikisha mtoto wake anamaliza shule ili awe na maisha bora hapo baadaye,” alisema Waziri Mkuu.

“Nirudie kuwakumbusha wazazi kwamba mtoto wa mwenzio ni mtoto wako, huwezi kukubali maisha yaharibike hivi hivi. Tuungane pamoja kuhakikisha tunashinda vita hii,” alisisitiza.

Waziri Mkuu leo anaendelea na ziara yake mkoani Mbeya kwa kutembelea wilaya ya Mbozi ambapo mbali ya kuzungumza na wananchi, atazindua maabara Vwawa sekondari, atakagua ghala la nafaka la NFRA na kupokea taarifa ya uzalishaji na usambazaji wa miche ya kahawa kwenye kituo cha TACRI - Mbimba.


IMETOLEWA NA
OFISI YA WAZIRI MKUU
JUMAPILI, MACHI MOSI, 2015

Thursday, February 26, 2015

PATO LA MWANANCHI MBEYA LAVUKA LENGO LA KITAIFA

     
                                                 
 WAZIRI MKUU Mizengo Pinda ameupongeza uongozi wa mkoa wa Mbeya kwa kuvuka lengo la wastani wa pato la mwananchi kitaifa na kuwataka waendeleze kasi ya kupambana na umaskini kwa wakazi wa mkoa huo.

Ametoa pongezi hizo jana usiku (Jumanne, Februari 24, 2015) wakati akizungumza na viongozi wa mkoa huo na wilaya zote wakiwemo wadau mbalimbali na viongozi wa dini mara baada ya kupokea taarifa ya Mkoa wa Mbeya.

Alisema katika mipango yake, Serikali ililenga kwamba pato la mtu kwa mwaka liwe sh. 1,186, 200, lakini kwa sababu ya jitihada mbalimbali mkoa huo umelivuka. “Katika taarifa aliyonisomea, Kaimu Mkuu wa Mkoa amesema wastani wa pato la mwananchi umeongezeka kutoka sh. 711,201/- mwaka 2008 hadi kufikia sh 1,420,427/- mwaka 2013 na kwamba mkoa unachangia asilimia 7.43 ya Pato la Taifa,” alisema.

Alisema kipato cha mtu mmoja kwa siku ni sh. 3,891/- ambazo ni zaidi ya Dola mbili za Marekani (sh. 3,400/-). “Wakubwa hawa wanatupima kwa kuangalia kipato cha mtu kwa siku. Wanasema nchi ni maskini iwapo watu wake wanaishi chini ya dola moja kwa siku (sawa na sh. 1,700/-).”

“Mbeya imeendelea kushika nafasi ya tatu kwa kuchangia vizuri Pato la Taifa ikiwa imetanguliwa na Dar es Salaam na Iringa. Ninawapongeza kwa sababu mmevuka malengo ya Taifa katika eneo la pato la mtu mmoja mmoja,” alisema Waziri Mkuu.

Mapema, Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Bw. Deodatus Kinawilo ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Chunya, alisema pato la mkoa limeongezeka kutoka sh. trilioni 1.779 mwaka 2008 na kufikia sh. trilioni 3.951 mwaka 2013. 

“Uchumi wa mkoa huu unategemea kilimo, ufugaji, uchimbaji madini, uvunaji mazao ya maliasili, biashara, uzalishaji viwandani na ajira katika taasisi za serikali na sekta binafsi,” alisema.

Wakati huohuo, uongozi wa mkoa wa Mbeya umetakiwa kuongeza bidii ili uweze kuinua kiwango cha ufaulu wa elimu ya kwa sababu umekuwa ukiendelea kushuka na kuwa chini ya kiwango cha asilimia 60 kilichowekwa na Serikali.

Waziri Mkuu aliutaka uongozi huo ubuni mbinu za kisomi zitakazowawezesha wanafunzi wa shule za msingi kuelewa wanachofundishwa, hivyo, kufaulu mitihani yao vizuri. ”Ufaulu wenu kwa shule za msingi ni asilimia 46.6, uko chini ya kiwango cha kitaifa cha ufaulu kwa asilimia 13.4. Ni matokeo yasiyoridhisha, fanyeni utaratibu maalum ili yapande,” alisema.

(mwisho)

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
JUMATANO, FEBRUARI 25, 2015.


Wednesday, February 25, 2015

MKUU MPYA WA WILAYA YA MISENYI AAPISHWA

 Mkuu wa wilaya ya Bukoba, Jaskon Msome kulia kabla alikuwa mkuu wa wilaya ya Musoma.
 Mkuu mpya wa wilaya ya Misenyi, Fadhil Nkurlu kulia, kabla ya kuapishwa.
 Baadhi ya viongozi wa dini walioudhuria sherehe ya kuapishwa kwa mkuu mpya wa wilaya ya Misenyi.

 Baadhi ya wajumbe wa kamati ya ulinzi na usalama ya mkoa wa Kagera.