Monday, September 30, 2013

JESHI LA POLISI LAJIZATITI KUTOKOMEZA AJALI

 Kamanda jeshi la polisi mkoani Kagera, Philip Kalangi.
 Mkuu wa kikosi cha usalama barabarani wa wilaya ya Bukoba, William Mkonda akitoa elimu juu ya masuala ya usalama barabarani kwa wanafunzi wa shule ya sekondari ya Bukoba iliyoko katika manispaa ya Bukoba.




Sunday, September 29, 2013

KUFUNGIWA MAGAZETI – WAHAFIDHINA SASA WANAONGOZA


Zitto Kabwe, Mb
Kwa mshtuko na masikitiko makubwa kuanzia jana jioni tumepokea taarifa za kufungiwa kwa magazeti mawili ya kila siku hapa nchini ya Mwananchi na Mtanzania. Serikali imechukua uamuzi huo kwa kutumia sheria ya kidikteta ya magazeti ya mwaka 1976 ambayo Tume ya Jaji Francis Nyalali iliiorodhesha kama sheria kandamizi. Sababu zilizotolewa kuhalalisha uamuzi huu ni sababu zisizo na maana na ambazo Serikali ingeweza kufungua mashtaka ya kawaida kabisa mahakamani kushtaki magazeti hayo iwapo haikupendezwa na habari walizochapisha.
Moja ya sababu ya kufungiwa kwa gazeti la Mwananchi ni kuchapisha taarifa kuhusu mishahara ya Serikali. Serikali inasema habari hii ni siri. Serikali hii hii ambayo imesaini makubaliano ya kuendesha serikali kwa uwazi (Open Government Initiative) na kumwagiwa sifa na Rais Barack Obama wa Marekani inalifungia gazeti kwa kuandika habari za mishahara ya watumishi wa Serikali. Mishahara kuanzia mshahara wa Rais mpaka wa mtendaji wa Kijiji haipaswi kuwa jambo la siri. Kuonyesha kuwa jambo hili linapaswa kuwa wazi mkutano ujao wa Bunge tutatafuta kila namna kutaja mshahara wa Rais, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu na baadhi ya Watendaji wa Mashirika makubwa ya Umma kama njia ya kuwaunga mkono gazeti la Mwananchi kwa habari yao hiyo. Mapato ya Mbunge yanajulikana sasa kuwa ni shilingi milioni 11.2 kwa mwezi kabla ya kuongeza posho za vikao za shilingi laki 200,000 kwa siku na posho ya kujikimu ya shilingi 130,000 kwa siku. Watanzania wana haki ya kujua wanawalipa kiasi gani watumishi wao. Tutaanza na mshahara wa Rais!
Gazeti la Mtanzania limefungiwa pamoja na mambo mengine kwa kuandika 'mapinduzi ni lazima'. Inashangaza Serikali ya Chama cha Mapinduzi inaogopa neno mapinduzi. Marehemu Mzee Steven Salum Nandonde, aliyekuwa mbunge wa Jimbo la Tandahimba alipata kusema bungeni kuwa 'lazima nchi ipinduliwe'. Ni matumizi ya lugha tu. Mzee Nandonde yeye alikuwa analalamikia maendeleo duni ya mikoa ya kusini na kutaka Kaskazini iwe Kusini na Kusini iwe Kaskazini. Serikali inafungia gazeti kwa sababu ya kuandika Mapinduzi ni lazima ilhali kila siku Zanzibar wanasema Mapinduzi daima!
Gazeti la Mtanzania linahaririwa na Absalom Kibanda, mwandishi wa habari ambaye bado anaponya majeraha ya mwili na kisaikolojia ya kuteswa na watu ambao mpaka leo hawajakamatwa. Badala ya Serikali kuwakamata watesaji wa Kibanda, inamnyima kazi Kibanda ili ateseke kwa njaa kwa kukaa miezi mitatu bila kazi. Pia wanatutesa Watanzania kwa njaa ya kupata habari ambayo ni haki ya msingi ya kikatiba. Hii ndio zawadi Serikali inampa Kibanda baada ya kung'olewa kucha, kunyofolewa jicho, kukatwa vidole na kuteswa kwa namna isiyoelezeka.
Matukio ya hivi karibuni na namna Serikali inavyoyachukulia yanaonyesha dhahiri kwamba Rais Kikwete kazidiwa nguvu na kundi la wahafidhina ndani ya chama na Serikali yake. Rais ambaye alianza kwa kuhubiri uvumilivu wa hali ya juu na hata yeye mwenyewe kupata kusema uvumilivu huu wengine wanauona kama udhaifu lakini ameamua kujenga Taifa la kuvumiliana. Rais alipata kulalamika hadharani kwamba kuna wenzake wanataka aongeze ukali. Ni dhahiri kundi hili la wahafidhina sasa ndio linalomwongoza Rais Jakaya Kikwete. Kitu kimoja tu Rais azingatie, kundi hili linaongozwa na maslahi binafsi ya kubakia kwenye utawala wakati yeye anapaswa kuacha 'legacy'. Rais Kikwete asipokuwa makini atakuwa Rais karatasi (lame duck) tu tunapoelekea mwisho wa utawala wake. Maamuzi ya hovyo na ya kidikteta ya kufungia magazeti yanamchora vibaya mbele ya wananchi na jamii ya kimataifa. Wahafidhina kuwa nguvu zaidi ya kiutawala ni makosa ambayo watanzania hawapaswi kuyakubali kamwe.
Wananchi sasa waifanye Serikali kujutia uamuzi wake wa kufungia magazeti. Nimeamua mimi binafsi kama mbunge kesho Jumatatu tarehe 30 Septemba, 2013 kupeleka taarifa rasmi kwa Katibu wa Bunge ya kupeleka muswada Bungeni wa kuifuta kabisa Sheria kandamizi ya magazeti ya mwaka 1976. Sasa tupambane na kundi dogo la wahafidhina ndani ya Serikali na CCM wasiopenda mabadiliko na iwe fundisho kwa wahafidhina wengine wowote waliopo ndani ya Serikali au nje ya Serikali kwamba Uhuru wa habari sio jambo la kuchezea kama golori.

Katiba ni Mwafaka wa Kitaifa. Viongozi zungumzeni

Kwa takribani wiki tatu sasa kumekuwa na sintofahamu kuhusu muswada wa sheria uliopitishwa na Bunge ili kufanya marekebisho ya sheria ya marekebisho ya Katiba ya mwaka 2011. Mjadala na upitishaji wa sheria hii uliweka rekodi ya pekee katika nchi yetu kwa vitendo vya kihuni kutokea Bungeni ambavyo nisingependa kuvirejea kutokana na aibu kubwa ambayo Bunge liliingia. Kiukweli kuna sintofahamu katika nchi kuhusu kuandikwa kwa Katiba mpya. Hii imechangiwa na kurushiana maneno miongoni mwa wanasiasa wa pande zote mbili, wanaopinga muswada ulivyo na wanaounga mkono muswada ulivyo. Masuala ya Tume imalize kazi yake lini, ushiriki wa Zanzibar na idadi ya wajumbe kutoka Zanzibar kwenye Bunge la Katiba, Wajumbe wa Bunge Maalumu wanapatikanaje na kadhalika ni masuala ambayo yanaweza kupatiwa mwafaka kwa viongozi kukaa na kuzungumza. Haya sio masuala ya kushindwa kujenga mwafaka labda kuwe na nia mbaya dhidi ya mchakato wa kuandika Katiba mpya. Katiba sio suala la kufanyia siasa. Katiba ni uhai wa Taifa.
Ni wazi kuna kundi kubwa ambalo halijitokezi waziwazi ambalo lingependa pasiwe na katiba mpya ya Wananchi. Kuna kundi lingine ambalo lingependa mchakato wa kuandika Katiba uendelee kwa miaka mingine zaidi ili kuweza kupata Katiba bora. Kuna kundi la Wabunge ambao kwa chinichini wanataka mchakato uendelee, uchaguzi uahirishwe mpaka mwaka 2017 na wao waendelee kuwa wabunge. Naamini watu hawa wanaota ndoto za mchana kwani hakuna mahusiano yeyote kati ya uchaguzi mkuu na kuandika katiba mpya. Kama Bunge hili la sasa na Serikali hii itashindwa kukamilisha zoezi hili, Bunge linalokuja na Serikali itakayoingia madarakani itaendelea nalo. Hivyo sio lazima kupata Katiba mpya kabla ya uchaguzi mkuu wa 2015. CHADEMA imependekeza kuwepo na marekebisho ya mpito kwenye Katiba ya sasa ili kuwezesha Tume huru ya Uchaguzi, masuala ya wagombea binafsi na kadhalika. Vyama vingine vya siasa vinaweza kuwa na mapendekezo yao ya mpito na hivyo kutoa nafasi ya kutosha kabisa wa kuandika Katiba makini.
Changamoto kubwa sana ya siasa za Tanzania ni kelele. Wanasiasa hatuzungumzi kwenye masuala yanayohusu uhai wa Taifa. Kila chama kinakuwa na misimamo yake na kuishikilia na hatimaye kujikuta tunapoteza fursa ya kuzungumza na kujadiliana kama Watanzania. Mwaka 2011 hali ilikuwa hivi hivi mpaka kundi la Wazee viongozi wastaafu walipoingilia kati na kupelekea wanasiasa kukaa na kuzungumza. Bahati mbaya sana viongozi wale ndio sasa wamepewa usukani wa kuandika Katiba kwa kuwa kwenye Tume. Hawawezi tena kufanya kazi ile ya kutafuta suluhu iliyopelekea Rais kuzungumza na viongozi wa vyama vyote vya siasa ikulu jijini Dar es Salaam.
Vyama vya Upinzani nchini sasa vimeungana kupinga muswada wa marekebisho ya Sheria ya Marekebisho ya Katiba ya mwaka 2011. Waziri wa Sheria na Katiba, Waziri wa Nchi ofisi ya Rais mahusiano na Uratibu, viongozi waandamizi wa CCM wote nao wameungana kuunga mkono muswada kama ulivyo. Badala ya kutafuta mwafaka, kumekuwa na kurushiana maneno ya kejeli na kadhalika. Taifa halijengwi namna hii. Taifa linajengwa kwa mwafaka na Katiba ni moja ya nyenzo wa Mwafaka wa Taifa. Niliwahi kuandika huko nyuma kuwa Katiba haiandikwi barabarani bali huandikwa mezani kwa watu kukaa na kukubaliana masuala ya Taifa dhidi ya maslahi ya kivyama ya wanasiasa.
Hakuna kilichoharibika. Bado tunayo nafasi kama Taifa kukaa na kukubaliana. Kwa hali ya sasa nafasi hii ipo mikononi mwa Mkuu wa Nchi, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Rais ana wajibu wa kikatiba wa kuhakikisha umoja wa kitaifa unaendelea kuongoza mchakato huu wa katiba ya nchi yetu. Hata hivyo ni vizuri kutahadharisha kuwa sio sahihi kwa wanasiasa wa pande zote kujaribu kumlazimisha Rais kuridhia ama kutoridhia sheria hiyo. Si sawa kisiasa kwa wanasiasa wa upinzani kujaribu kumlazimisha Rais ambaye pia ni Mwenyekiti wa chama chenye wabunge wengi bungeni kwenda tofauti na wabunge wake na wakati huohuo ni utovu wa nidhamu kwa Waziri wa Sheria kujaribu kumshauri hadharani Rais wake kuridhia sheria hiyo kwani ni kinyume cha misingi ya uongozi na pia kinatafsirika kama kumshurutisha (blackmail) Rais wake.
Kutosaini muswada huu kunaweza kuleta mgongano kati ya Wabunge wa CCM na Rais. Hata hivyo Rais lazima aweze kushawishi chama chake kwamba umoja wa kitaifa ni muhimu ziadi kuliko maslahi ya kisiasa ya chama chao. Pia kikatiba Rais anasaini miswada kuwa sheria akiwa Mkuu wa Nchi na sio Mkuu wa Serikali ya Jamhuri. Akiwa Mkuu wa Nchi maslahi mapana ni kuweka mwafaka wa pamoja miongoni mwa wananchi. Rais Jakaya Kikwete anapaswa kutumia mamlaka yake kama Mkuu wa Nchi kuiweka nchi pamoja kwa kuurejesha muswada bungeni ili uweze kujadiliwa upya na wadau wote na kupitishwa tena na Bunge. Ibara ya 97 ya Katiba ya sasa imeweka masharti ya utaratibu wa kutunga sheria na iwapo Rais ataurudisha muswada huu Bungeni pamoja na maelezo ya hatua hii, upitishwaji wake utahitaji theluthi mbili ya wabunge wote. Hii itakuwa hatua muhimu sana katika historia ya demokrasia yetu. Rais afuate ushauri huu kwani una manufaa makubwa.
Hata hivyo, ni lazima pawepo na mazungumzo miongoni mwa wanasiasa na makundi ya kijamii kuhusu Katiba. Katiba nzuri itapatikana pale tu ambapo mazingira ya kisiasa yanaonyesha nia njema kwa pande zote kisiasa. Kukwepa kuangaliana machoni na kuzungumza tofauti zetu za kimitazamo ni hatari zaidi. Juzi ngumi zimerushwa Bungeni. Kesho zitakua mitaani na vijijini kwetu. Tunataka kujenga Taifa la namna hiyo?

KONGAMANO LA UWEZESHAJI WA MIKOA YA KASKAZINI

  Baadhi ya Washiriki wa Kongamano la uwekezaji kwa  mikoa ya Kanda ya Kaskazini wakimsikiliza Waziri mkuu, Mizengo Pinda wakati alipofungua kongamano lao kwenye hoteli ya Mkonge mjini Tanga , Septemba 26, 2013. (Picha na ofisi ya Waziri Mkuu)

Waziri Mkuu, Mizengo Pinda akitazama sketi  iliyoshonwa  kwa mtindo wa vazi la asili la watu wa Hanang wakati  alipotembelea banda la Wilaya hiyo katika maonyesho  yaliyoambatana na  Kongamano la Uwekezaji la Kanda  ya Kaskazini lililofunguliwa na Waziri Mkuu kwenye hoteli ya Mkonge Mjini Tanga Septemba 26, 2013.  Kushoto ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mku, Uwezeshajina Uwekezaji ambaye pia ni Mbunge wa Hanang, Dr.Mary Nagu, Wapili Kulia ni  Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Chiku Galawa na wapili kulia ni Mkuu wa WIlaya ya Hang, Christina Mdeme. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

Thursday, September 26, 2013

WAZIRI MKUU PINDA WILAYANI NGORONGORO

  Mke wa Waziri Mkuu,mama Tunu Pinda  akimbeba mmoja wa watoto  waliofika na wazazi wao katika Hospitali Tuele ya Wilaya ya Ngorongoro  ya Wasso iliyopo Loliondo Sepyemba 23,2013. mama Pinda alifuatana na Mheshimiwa  waziri Mkuu, Mizengo Pinda katika ziara ya wilaya  ya Ngorogoro. (Picha na Ofisi ya waziri Mkuu)

 Waziri Mkuu, Mizengo Pinda akisalimian ana wananchi wa  Kijiji cha Engosero wilayani Ngorongoro  kabla ya kuzungumza nao kijijini hapo Septemba 24, 2013. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

 Mke wa Waziri Mkuu, Mama Tunu Pinda akisalimiana na Mganga Mkuu wa Hoapitali Teule ya Wilaya na Ngorongoro ya Wasso, Dr. Padri  Franco Manent  kabla ya kuitembelea akiwa katika ziara ya wilaya hiyo Septemba 24, 2013. (Picha na Ofisi ya Waziri  Mkuu)

MAKOMANDO WA KENYA

Makomando wa nchi ya Kenya wakifanya vitu vyao

Wataalamu watafuta miili Westgate


Jengo la Westgate ambalo ghorofa zake tatu ziliporomoka
Vikundi vya maafisa wa uchunguzi wa mauaji vinatafuta miili ya mateka waliouawa ndani ya jengo la Westgate ambao idadi yao haijulikani.
Mateka walizuiliwa na magaidi kwa siku nne kabla ya serikali kutangaza kumalizika rasmi kwa shambulizi hilo
Zaidi ya watu 65 waliuawa na mamia ya wengine kujeruhiwa.
Waziri wa usalama Joseph Ole Lenku amesema kuwa hatarajii kuwa idadi ya waliofariki itaongezeka na kusema kuwa miili ya magaidi pakee ndio itapatikana ndani ya vifusi.
Hii ni baada ya sehemu ya jengo hilo kuporomoka wakati shughuli za uokozi zilikuwa zinaendelea .
Lakini kwa mujibu wa shirika la Red Cross, watu 61 wangali hawajulikani waliko.
Wakati huohuo, Kenya inaendelea na siku tatu za maombolezi ya vifo vya raia na baadhi ya maafisa wa usalama waliofariki katika shambulizi hilo.
Mazishi ya mtangazaji mmoja wa Televisheni na Redio, Ruhila Adatia yalifanyika siku ya Alhamisi.
Bendera zingali zinapeperushwa nusu mlingoti kwa heshima ya wale waliofariki.
Walinzi walionekana wakichunguza abiria kabla ya kuabiri magari ya usafiri.
Huku wasiwasi ukiongezeka miongoni mwa wakenya kuhusu hali ya kujiandaa kwa maafisa wa usalama kuhusiana na mashambulizi kama haya, taarifa zinasema kuwa serikali inajiandaa kudurusu mikakati yake ya kupigana dhidi ya ugaidi na majanga mengine.
Kundi la kigaidi la Al Shabaab linasema limeshambuli Kenya kutokana na nchi hiyo kujihusisha na vita dhidi ya kundi hilo nchini Somalia

Wednesday, September 25, 2013

WAZIRI MKUU PINDA AKAGUA GFHALA LA MAHINDI

 Waziri Mkuu, Mizengo Pinda akikagua akiba ya mahihindi wakati  alipotembelea   Maghara ya Kitengo cha  Usalama wa Chakula, (NFRA) mjini Arsha Septemba 25, 2013. Kushoto kwake ni Naibu Waziri wa Kilimo,  chakula   na Ushirika, Adam Malima. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)


Waziri Mkuu, Mizengo Pinda na Mkewe Tunu (kushoto)  wakitazama ngoma kutoka katika kikundi cha sanaa cha Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) baada ya kuwasili kwenye uwanja wa ndege wa Tanga Septemba 25, 2013. Mheshimiwa Pinda anatarajiwa kufungua Kongamano la Uwekezaji la Kanda ya Kaskazini  Mjini Tanga Septemba 26, 2013.(Picha na  Ofisi ya Waziri Mkuu)

WAZIRI MKUU PINDA WILAYANI NGORONGORO

 Waziri Mkuu, Mizengo Pinda akisaliiana na Ambilikile Mwasapila maarufu kwa jina la Babu  wakati alipopita katika kijiji cha Samunge akilelekea Digodigo kuhutubia mkutano wa hadhara Septemba 24, 2013. Alikuwa katika  ziara ya wilaya  ya Ngorongoro . (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)


   Waziri Mkuu, Mizengo Pinda akihutunia Mkutano wa hadhara katika kijijicha Digodigo wilayani  Ngorongoro  Septemba  24, 2013.  Kulia ni Mkewe Tunu na kushoto  ni Mkuu wa mkoa wa Arusha  Mulugo. (Picha na Ofisi ya wazir Mkuu)


Monday, September 23, 2013

ICC yamruhusu William Ruto kurejea Kenya



Ruto alifikishwa ICC kwa tuhuma za uhalifu dhidi ya binadamu
Majaji katika mahakama ya kimataifa kuhusu uhalifu wa kivita ICC wameahirisha kesi ya naibu Rais wa kenya William Ruto kwa juma moja ili kumpa mda kurejea nyumbani kushughulikia hali ya kiusalama inayokumba taifa hilo.
Watu wanoaminika kuwa magaidi wa Al Shabaab wameteka jumba la kifahari lenya maduka la Westgate jijini Nairobi na kuwazuilia mateka wakenya kadhaa.
Bwana Ruto anakabiliwa na mashtaka ya uhalifu wa kibinadamu kufuatia ghasia za baada ya uchaguzi wa 2007 nchini kenya.
Ruto na Rais Uhuru Kenyatta, wanakabiliwa na tuhuma za za uhalifu dhidi ya binadamu baada ya kudaiwa kuhusika na ghasia za kikabila baada ya uchaguzi wa mwaka 2007-2008 ambapo watu zaidi ya elfu moja waliuawa.
Mahakama iliakhirisha kesi baada ya kikao cha dharura kuitishwa huku upande wa mashtaka ukisema kuwa hauna pingamizi lolote ikiwa kesi zitaakhirishwa kwa muda mfupi.
Mwakilishi mmoja wa mashahidi aliangua kilio mahakamani na kutaka mahakama iweze kumruhusu Ruto kurejea nyumbani kushughulikia swala hilo la dharura.
''Kutokana na hali ilivyo na maoni tuliyoyasikia , mahakama inamruhusu Ruto kurejea nyumbani kwa muda wa wiki moja,'' alisema jaji anayesimamia kesi hiyo, Chile Eboe-Osuji.
"Kwa sasa Ruto ataruhusiwa kusalia Kenya kwa wiki moja, ila ikiwa atatoa ombi lengine,'' alisema jaji Chile.
Kwa mujibu wa wakili wa Ruto,Karim Khan, alitarajiwa kuondoka Uholanzi saa tatu asubuhi, saa za Afrika Mashariki

Westgate:Mlipuko na moshi mkubwa


Jeshi la Kenya linasema kuwa limedhibiti jengo hilo ingawa hali bado ni mbaya
Huku hali ya mshikemshike ikiendelea kushuhudiwa katika jengo la Westgate lenye maduka, ufyatulianaji risasi umesikika ndani ya jengo hilo lenye maduka na mikahawa zaidi ya themanini.
Milio hiyo ilidumu kwa dakika tatu na kufuatiwa na moshi mkubwa juu ya jengo hilo. Hakuna taarifa kamili kuhusu kilichosababisha moshi huo.
Wapiganaji wa Al shabaab wamewateka nyara raia ambao idadi yao haijulikani. Walikuwemo ndani ya jengo wakiendelea na shughuli zao kuanzia Jumamosi mchana wakati wapiganaji wa Al shabaab walipowavamia na kuanza kufyatua risasi kiholela.
Inaarifiwa kuna maiti kumi katika ghorofa ya kwanza ya jengo hilo.
Aidha wapiganaji hao wanaoaminika kuwa wanachama wa Al Shabaab ni kati ya kumi na kumi na watano na bado wangali ndani ya jengo hilo.
Ripoti zinasema kuwa ufyatulianaji mkubwa wa risasi pamoja na milipuko imesikika katika jengo hilo kwa takriban dakika 15.
Harakati za kuendelea kumaliza operesheni hiyo zinaendelea lakini hali ya mateka walio ndani ya jengo hilo inaendelea kudorora.
Wakenya waliofanikiwa kuondoka katika jengo la Westgate kwa usaidizi wa polisi
Rais Kenyatta amesema kuwa jeshi linajitahidi kuhakikisha kuwa linakabiliana vilivyo na wanamgambo hao.
Helikopta za polisi zinazunguka juu ya jengo hilo pamoja na ndege za kijeshi kushika doria. Vikosi vya usalama vinaendelea na operesheni kujaribu kuwanusuru waathiriwa wakati hali ikiwa ni ya ati ati katika eneo la shambulizi.
Awali jeshi la Kenya lilisema limeweza kudhibiti jengo hilo lote ingawa bado limetaja hali kuwa tete mno hasa katika kujaribu kuwaokoa mateka waliosalia ndani ya jengo hilo.
Ripoti zinasema kuwa watu 69 wamefariki katika shambulizi hilo la Al Shabaab kufikia sasa huku 175 wakijeruhiwa. Baadhi wametibiwa na kuondoka hospitalini. Baadhi ya majeraha waliyopata ni majereha ya risasi na kutokana na guruneti ambalo Al shabaab waliwarushia wale waliokuwa ndani ya mikahawa siku ya Jumamosi.
Kundi hilo limekiri kutekeleza shambulio hilo kutokana na hatua ya Kenya kupeleka majeshi yake nchini Somalia ili kukabiliana na wapiganaji hao.

Vikosi vya usalama vinaendelea na juhudi za kukabiliana na magaidi walioteka nyara baadhi ya wakenya katika jengo la Westgate

Vikosi vlama vinaendelea na juhudi za kukabiliana na magaidi walioteka nyara baadhi ya wakenya katika jengo la Westgateya usa
Katika ukurasa huu tutakupasha moja kwa moja matukio yanavyojiri katika jengo la Westgate.
Ikiwa uko karibu na jengo hilo unaweza kutupasha hali unavyoiona kupitia kwa ukurasa wetu wa Bofya f

15:33 Waziri wa usalama wa Kenya Joseph Ole Lenku asema kuwa wanajeshi wameweza kudhibiti jengo lote la Westgate
15:20 Polisi waonekana wakikimbia huku na kule katika harakati zao hizo dhidi ya Al Shabaab
Juhudi za uokozi Westgate
14:56 Mkuu wa majeshi Meja Jenerali Julius Karangi amesema magaidi hao wanaweza kujisalimisha ikiwa wanataka kwa sababu jeshi litakabiliana nao vilivyo. Pia amesema kuwa Kenya inakabiliana na magaidi wa kimataifa

14:35 Ole Lenku anasema kuwa hali ingali tete lakini vikosi vya usalama vya Kenya vinakaribia kuwazingira magaidi hao...Hadi kufika sasa watu 62 wamefariki na wengine zaidi ya 175 kujeruhiwa. Pia ameongeza kuwa magaiodi wote ni wanaume, kutokana na taarifa za awali kuwa magaidi hao walikuwa wanaongozwa na mwanamke

14:30 Ole Lenku anasema kuwa wanajeshi kumi wamejeruhiwa na wanapokea matibabu. Pia mateka karibu wote wameweza kuokolewa. Ole Lenku pia amesema kuwa wameweza kuwaua magaidi wawili

14:28 Waziri wa usalama Joseph Ole Lenku anasema kuwa moshi ulitokana na moto uliosababishwa na magaidi wlaioko ndani ya jengo hilo kujaribu kusambaratisha juhudi za wanajeshi wa Kenya dhidi yao

Moshi mkubwa ukitoka ndani ya jumba la Westgate
14:03 Mkuu wa polisi David Kimaiyo asema kuwa vikosi vya usalama vinakaribia kudhibiti jengo hilo lote na vimeingia ndani kabisa ya jengo hilo kiasi cha kuwaokoa baadhi ya mateka
14:00 PM: Milipuko zaidi yasikika katika jengo hilo

13:54: Mwandishi wa BBCIdriss Situmaaliye katika eneo la Westgate anasema duru zinaarifu kuwa vikosi vya usalama vya Kenya vinasema kuwa ndivyo vimelipua sehemu ya jengo kujaribu kuingia ndani kabisa ya jengo hilo
13:52 PM Magari ya Ambulance yaobnekana yakienda katika eneo la shambulizi pamoja na magari ya zima moto. Vikosi vya usalama vinawataka watu kuondoka karibu na eneo la operesheni hiyo ili kuwawezesha kufanya kazi yao

Waathiriwa wa shambulizi la Westgate
13:49 pm: Moshi mkubwa mweusi waonekana ukitoka juu ka juu katika jengo hilo haijulikani nini kilichosababisha
13:19 pm Moshi mkubwa unaonekana ukitoka katika jengo la Westgate ambako wapiganaji wa Al Shabaab wanawazuilia mateka wakenya ambao idadi yao haijulikani

UFUNGUZI WA WIKI YA NENDA KWA USALAMA MKOANI KAGERA

 Wanafunzi wa shule ya kolping waliokuwa na shughuli ya kupiga tarumbeta wakati wa sherehe za maadhimisho ya wiki ya nenda kwa usalama zilizofanyika kwenye viwanja vya kaitaba.
 Maofisa wa jeshi la polisi kitengo cha usalama barabarani wakijiandaa kuonyesha mambo yao kwa vitendo.


 Mkuu wa mkoa wa Kagera Kanali mstaafu Fabian Massawe wa tatu toka kushoto akipokea maandamano.
 Baadhi ya viongozi wa serikali.

 Kikosi cha zimamoto hakikubaki nyuma.



SERIKALI KUPELEKA MAGUNIA 200,000 YA MAHINDI NGORONGORO - WAZIRI MKUU






WAZIRI MKUU Mizengo Pinda amesema Serikali itahakikisha inawapatia chakula cha uhakika wakazi wa Tarafa ya Ngorongoro wakati ikiendelea kutafuta ufumbuzi wa kudumu kwa wakazi wanaoishi ndani ya Hifadhi ya Ngorongoro ili waweze kujikimu.

Amesema ili kukabiliana na tatizo la njaa linalowakabili wakazi wa tarafa hiyo, kwa kuanzia Serikali itaipatia kila kaya magunia matano kila baada ya miezi sita wakati ikitafuta suluhisho la kudumu la tatizo la njaa linalowakabili wakazi hao wanaokadiriwa kufikia kaya 20,000.

Ametoa kauli hiyo jana jioni (Alhamisi, Septemba 19, 2013) wakati akizungumza na wakazi wa kata saba za Tarafa ya Ngorongoro katika mkutano wa hadhara uliofanyika Enduleni Madukani wilayani Ngorongoro mkoani Arusha.

Alikuwa akijibu maswali yaliyoulizwa na wakazi zaidi ya 10 wa tarafa hiyo ambao walipewa fursa ya kuuliza maswali ambapo wengi wao walitaka Serikali iwaruhusu kulima mashamba ya kujikimu katika maboma wanayoishi ambayo yamo ndani ya Hifadhi ya Ngorongoro.

“Nimelitazama jambo hili kwa kina, najua wengi mnataka kusikia habari ya kulima kwenye mashamba ya kujikimu lakini mimi nina pendekezo la tofauti. Serikali ichukue hatua ya kuwapatia chakula cha uhakika wakati jambo hili likiangaliwa kwa undani katika ngazi mbalimbali,” alisema.

“Nimeelezwa kuwa kuna kaya karibu 20,000 na kila kaya ina watu karibu watano hadi sita, tukiamua kutoa magunia matano kwa miezi sita ni sawa na tani 10,000 na miezi sita mingine tukawapa magunia matano tutakuwa tumetatua tatizo la njaa kwa kila kaya. Hili ni jambo ambalo Serikali inaweza kulifanya kwa sababu mmetusaidia kutunza hifadhi hii,” alisema.

Waziri Mkuu aliwaahidi wakazi hao kwamba suala la kuwa na mashamba madogo ya kujikimu litajadiliwa kwa pamoja baina ya Baraza la wafugaji na Bodi ya Ngorongoro ambayo inatarajiwa kutangazwa hivi karibuni.

“Suala la mashamba ya kujikimu halitaki kutolewa kauli za pupa, inabidi tukae na Baraza la Wafugaji tuone tunapataje njia ya kudumu ya kutatua tatizo hili. Kila aliyekuja hapa anataka shamba la kujikumu nilipodadisi nikapata picha kuwa ni mashamba madogo. Sasa ni lazima tukae na Malaigwanan na Baraza lenu ili tujue kama tunaruhusu mashamba ni ya ukubwa gani na ni mazao gani yalimwe katika hayo mashamba...,” alisisitiza.

Aliwakumbusha wakazi hao umuhimu wa kutunza hifadhi hiyo ya Ngorongoro ambayo imejizolea sifa duniani kote na imepata fursa ya kuwa miongoni mwa maajabu saba ya dunia katika Bara la Afrika.

Waziri Mkuu ambaye yuko mkoani Arusha kwa ziara maalum ya kusikiliza matatizo ya ardhi yanayowakabili wakazi wa wilaya ya Ngorongoro, kabla ya kuhutubia mkutano huo aliamua kukutana na Baraza la Wafugaji pamoja na wazee wa kimila (Malaigwanan) na kusikiliza baadhi ya kero kutoka kwa wazee hao.

Waziri Mkuu alisema anatambua taabu inayowapata wakazi hao kwani katika tathmini iliyofanyika mwezi Julai hadi Agosti 2013 juu ya hali ya watu na uchumi katika tarafa ya Ngorongoro imebainika kuwa tarafa hiyo inakabiliwa na umaskini wa kipato unaosababishwa kutegemea ufugaji kama njia kuu ya uchumi.

Kwa mujibu wa tathmini hiyo, tarafa ya Ngorongoro ina wakazi 87,851 kwenye jumla ya kaya 19,908 ikiwa na idadi ya ng’ombe 131,509; mbuzi 163,207 na kondoo 166,872. Hata hivyo, hali ya uchumi wa mifugo imeendelea kushuka kwani ni asilimia tatu (3%) pekee ya wenyeji wa Hifadhi ya Ngorongoro wanamiliki asilimia zaidi ya 80 ya mifugo yote iliyopo kwenye tarafa hiyo wakati asilimia 97 ya wenyeji ndio wanaomiliki asilimia 20 ya mifugo yote.

Tathmini hiyo ilifanyika ikiwa ni utekelezaji wa maelekezo ya Waziri Mkuu aliyoyatoa alipokutana na Malaigwanan pamoja na baadhi ya wajumbe wa Baraza la Wafugaji la Ngorongoro jijini Arusha na mjini Dodoma Juni mwaka huu.

Waziri Mkuu leo anaendelea na ziara yake wilayani Karatu na kesho atakwenda Weruweru, Moshi kwenye Jubilei ya miaka 50 ya shule hiyo ya sekondari.


(mwisho)

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
IJUMAA, SEPTEMBA 20, 2013.



--